Rais Samia mgeni rasmi siku ya uhuru wa vyombo vya habari duniani
- Maadhimisho hayo kufanyika Mei 1-3 jijini Arusha.
- Rais Samia kuwa mgeni rasmi.
- Uhuru wa kujieleza, maslahi ya wanahabari na teknolojia kutawala mijadala ya maadhimisho hayo.
Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan anatarajia kuwa mgeni rasmi katika kilele cha maadhimisho ya siku ya uhuru wa vyombo vya habari duniani huku maadhimisho hayo yakipambwa na shughuli mbalimbali ikiwemo mijadala inayolenga kuimarisha tasnia ya habari Tanzania.
Sherehe hizo kwa Tanzania, kitaifa zitafanyika kuanzia Mei 1 hadi 3, 2022 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC) jijini Arusha na kuwakutanisha wadau mbalimbali wa habari wa ndani na nje ya nchi.
“Sherehe za mwaka huu kutokana na ukubwa na umuhimu wake, wadau pamoja na Serikali waliona ni vema mkuu wa nchi aweze kuwa mgeni rasmi katika sherehe hizi,” amesema Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Habari – MAELEZO, Rodney Thadeus.
Thadeus aliyekuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma leo Aprili 19, 2022, amesema ni heshima ya pekee kwa tasnia ya habari Tanzania kwa sababu “kiongozi wa nchi anapoamua kuja kwenye jambo lako maana yake ameona kuna umuhimu kwenye hiyo sekta.”
Wadau waliamua Rais Samia awe mgeni rasmi kwa sababu tangu aingie madarakani amekuwa akihimiza uhuru wa vyombo vya habari huku akipenda kuona vinaimarika, wanahabari wanapata maslahi yao vizuri ili wachangie katika maendeleo ya nchi.
Zinazohusiana:
- LHRC yazungumzia adhabu ya vituo vitatu vya televisheni mtandaoni.
- Waziri Nape ayafungulia magazeti manne yaliyofungiwa
- CCM yazidi kuongeza umiliki wa vyombo vya habari Tanzania
Katika siku tatu za maadhimisho hayo jijini Arusha, kutakuwa na shughuli mbalimbali ikiwemo maonyesho ya kazi za waandishi wa habari, mijadala mbalimbali itakayohusu uhuru wa vyombo vya habari na kujieleza, jinsi ya kuikuza tasnia ya habari na kuboresha maslahi ya wanahabari.
Pia itaangalia namna Tehama inavyoweza kusaidia kuimarisha utendaji wa vyombo vya habari ili viwe na mchango mzuri kwenye maendeleo ya jamii.
Kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu ni “Vyombo vya Habari na Changamoto za Kidijitali”Maandalizi ya sherehe hizo yanaratibiwa na Kamati ya Kitaifa kwa kushirikiana na Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO).
Wadau wengine waliopo katika kamati hiyo ni kampuni ya habari na teknolojia ya Nukta Afrika, Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (Tamwa), Umoja wa Klabu ya Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) na Misa Tanzania.
Maadhimisho hayo yataambatana na kutoa tuzo 12 kwa wanahabari na vyombo vya habari ambavyo vimekuwa mstari wa mbele kutoa taarifa muhimu zinazochochea maendeleo kwenye jamii.
“Sherehe hizi zitakuwa za kimataifa kwa maana kutakuwa na ushiriki wa wageni kutoka nchi mbalimbali ambao wanafanya kazi katika sekta ya habari,” amesema Thadeus na kuongeza kuwa wageni hao watatoka katika nchi za Afrika na zitawajumuisha wadau wa maendeleo kikiwemo Chama Cha Wahariri wa Vyombo vya Habari Afrika Mashariki.
Latest
