Serikali yafuta tena sherehe za kitaifa za Uhuru wa Tanzania Bara
- Badala yake itaadhimishwa kwa kwa midahalo na makongamano wilayani.
- Pia itakuwa ni siku ya kufanya shughuli za kijamii ikiwemo usafi.
- Sh960 milioni za sherehe hiyo kujenga mabweni ya shule.
Dar es Salaam. Wakati zikiwa zimebaki siku chache Watanzania kuadhimisha Siku ya Uhuru wa Tanzania Bara, tukio hilo halifanyika kama ilivyozoeleka kwa sherehe ya kitaifa na gwaride badala yake kutakuwa na shughuli za kijamii na midahalo katika ngazi ya wilaya.
Kwa kawaida sherehe hizo ambazo huadhimishwa kila mwaka ifikapo Desemba 9 huadhimishwa katika uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam na kuambatana na shughuli mbalimbali ikiwemo haraiki ya vijana na gwaride la majeshi nchini.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu George Simbachawene amesema tukio hilo la kitaifa halitakuwepo.
Maadhimisho ya Sherehe za Miaka 61 ya Uhuru wa Tanzania Bara mwaka huu 2022 yatafanyika kwa midahalo na makongamano mbalimbali yatakayofanyika katika wilaya zote hapa nchini.
Matukio hayo yatajikita katika kujadili, kutafakari kwa pamoja na kukumbuka tulikotoka, tulipo na tunakoelekea kuhusu maendeleo endelevu ambayo nchi imeyafikia.
“Hivyo hakutakuwa na Gwaride na shughuli nyingine za Kitaifa,” amesema Waziri Simbachawene leo Desemba 5, 2022.
Maadhimisho ya mwaka huu yataadhimishwa kwa Kauli mbiu inayosema “Amani na Umoja ni Nguzo ya Maendeleo Yetu.”
“Makongamano hayo yatatanguliwa na ratiba mbalimbali kwa viongozi wa mikoa na wilaya kufanya shughuli za kijamii kama vile kufanya usafi katika maeneo ya hospitali, shule, nyumba za wazee na makundi yenye mahitaji maalum,” amesema.
Serikali imeelekeza ofisi zote za Serikali hapa nchini kupambwa kwa mapambo ya rangi za bendera ya Taifa pamoja na picha ya Rais Samia Suluhu Hassan.
Hii itakuwa mara ya kwanza kwa Rais Samia kufuta sherehe hizo tangu alipoingia marakani Machi 2021 huku mtangulizi wake Hayati Rais John Magufuli akifuta sherehe hizo mara tatu siku za uongozi wake.
Wakati wa Magufuli, sherehe hizo hazikuadhimishwa kitaifa mwaka 2015, 2018 na 2020 lakini mwaka jana zilifanyika kitaifa katika uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.
Zinazohusiana:
-
Rais Magufuli afuta sherehe za Uhuru kwa mara ya tatu
-
Rais Magufuli afuta sherehe za uhuru kwa mara ya pili
Fedha za sherehe kujenga mabweni
Fedha zilizokuwa zimetengwa na Wizara na taasisi kwa ajili ya Maadhimisho ya Sherehe za Uhuru mwaka huu zitapelekwe Ofisi ya Rais Tamisemi kwa ajili ya kujenga mabweni katika shule nane za msingi za wanafunzi wenye mahitaji maalum hapa nchini.
“Sh960 milioni zitatumika kujenga shule ya msingi Buhangija mkoani Shinyanga, Goweko (Tabora), Darajani (Singida), Mtanga (Lindi), Songambele (Lindi), Msanzi (Rukwa), Idofi (Njombe), na Longido mkoami Arusha,” amesema Simbachawene.
Amesema hatua hiyo imefikiwa ili kuwajali na kuwajengea mazingira rafiki watu wenye mahitaji maalum hapa nchini.