Rais Samia aungana na viongozi duniani kumlilia Malkia Elizebeth II
- Alifariki Septemba 8, 2022 akiwa na miaka 96.
- Atakumbukwa kwa kuwa nguzo ya amani, umoja na utulivu duniani.
Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan ameungana na viongozi mbalimbali duniani kuomboleza kifo cha Malkia wa Uingereza Elizabeth II aliyefariki jana huku wakisema atakumbukwa kwa kuwa nguzo ya amani na utulivu duniani.
Malkia Elizabeth aliyeshikilia kiti cha familia ya ufalme tangu mwaka 1952 amefariki Septemba 8, 2022 katika kasri la Balmoral nchini Uingereza alikokuwa akipatiwa matibabu.
Kupitia ukurasa wake wa Twitter Rais Samia ameeleza majonzi yake kwa kumpoteza kiongozi huyo ambaye alikuwa nguzo ya amani, umoja na utulivu duniani.
Nimesikitishwa na taarifa za kifo cha Malkia Elizabeth II. Kwa niaba ya Watanzania wote, natuma salamu za pole kwa Familia ya Kifalme @RoyalFamily na raia wote wa Uingereza. Malkia atakumbukwa duniani kote kama nguzo ya Amani, Umoja na Utulivu. pic.twitter.com/XsIpsYtG94
— Samia Suluhu (@SuluhuSamia) September 8, 2022
Malkia Elizabeth II (96) katika makazi ya Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, Oysterbay Jijini Dar es Salaam.
Taarifa za kifo cha Malkia Elizabeth zimegusa hisia za viongozi mbalimbali duniani ambao kwa pamoja wameungana na familia ya kifalme (Royal Family) kuomboleza kifo cha kiongozi huyo ambaye ameshika cheo cha malkia kwa miaka 70 mfululizo.
Waziri Mkuu wa Uingereza Liz Truss ambaye aliteuliwa na Malkia Septemba 6, 2022 amesema mfalme ndiye mwamba ambao Uingereza ya kisasa ilijengwa na kupitia ukurasa wake wa Twitter ameonyesha kuhuzunishwa kwake na kifo cha kiongozi huyo.
“Ni siku ya masikitiko makubwa, lakini Malkia Elizabeth II anaacha urithi mkubwa” amesema Truss.
Rais wa Marekani Joe Biden na mkewe Jill Biden wamehuzunishwa na msiba huo na kutoa pole kwa familia na watu wote ambao waliguswa na maisha ya Malkia Elizabeth.
“Mawazo yetu na maombi yetu kwa watu wote wa Taifa la Marekani yapo pamoja na watu wa Uingereza na watu wa jumuiya ya madola wakati huu wa maombolezo,” imesema taarifa ya Biden iliyotolewa jana.
Soma zaidi
“Maisha yaliyoacha alama”
Viongozi wa nchi za Afrika nao wameonyesha masikitiko yao kwa kumpoteza kiongozi huyo ambae enzi za uhai wake alitembelea nchi mbalimbali za Afrika ikiwemo Kenya.
“Tutamkumbuka kwa mahusiano mema aliyoyafurahia na nchi ya Kenya, kumbukumbu zake zitaendelea kutuhamasisha, tunaungana na Jumuiya ya Madola kuomboleza na kutoa pole kwa familia ya kifalme,” amesema Rais mteule wa Kenya William Ruto.
Kwa upande wake Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa amemtaja Malikia kama “mtu mashuhuri, aliyeishi maisha yaliyoacha alama”. Maisha yake na urithi wake utakumbukwa na wengi duniani kote,” ameeleza Rias huyo katika ukurasa wake wa Twitter kama sehemu ya kuonyesha masikitiko yake baada ya msiba huo.
Mpango wa kuuaga mwili na mazishi
Mazishi ya Malkia Elizabeth yanatarajiwa kufanyika huko Westminster Abbey ndani ya wiki mbili. Siku kamili itathibitishwa na Kasri la Buckingham.
Kabla ya mazishi, mwili wa Malkia utalazwa katika ukumbi wa Westminister kwa takriban siku nne.
Jambo hili hufanyika ili kuruhusu raia wa Uingereza kuutazama mwili wake na kuuaga kwenye ukumbi huo ambao unaaminika kuwa wa zamani zaidi ikilinganishwa na kumbi nyingine za Westminister.
Hata hivyo, kwa muda mrefu jengo hilo halijatumiwa kufanya maombolezo ya mazishi tangu aagwe mama yake Malkia mwaka 2002, ambaye ndiyo mtu wa mwisho wa familia ya Ufalme ya ufalme kuagwa.