Rais Samia atuma salamu za pole vifo vya watu 14 Simiyu
- Ajali hiyo imetokea baada ya magari mawili kugongana wilayani Busega.
- Watu 14 wafariki dunia wakiwemo waandishi wa habari watano.
- Rais Samia atoa pole kwa wafiwa.
Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan ametoa salamu za pole kwa wananchi ambao wamepoteza ndugu zao katika ajali ya barabarani iliyotokea mkoani Simiyu leo asubuhi na kugharimu maisha ya watu 14.
Kati ya watu waliofariki dunia, watano ni waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali huku wengine wakipata majeraha.
Watu hao wamefariki dunia baada ya gari la waandishi wa habari iliyokuwa kwenye msafara wa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza (RC), Robert Gabriel kugongana na gari ya abiria aina ya Toyota Hiace katika eneo la Nyamikoma, Wilaya ya Busega katika Mkoa wa Simiyu.
Rais Samia amesema ameshtushwa na kutokea kwa ajali hiyo ambayo imegharimu maisha ya watu muhimu kwenye jamii huku akiwataka Watanzania kuwaombea majeruhi wapone haraka.
“Poleni sana wafiwa wanahabari na jamaa wote. Mungu aziweke mahala pema peponi roho za marehemu na awajaalie majeruhi wapone haraka,” amesema Rais Samia.
Taarifa za awali zinaeleza kuwa waandishi wa habari walipoteza maisha katika ajali hiyo ni Husna Mlanzi kutoka kituo cha televisheni cha ITV, Vanny Charles (Icon), Antony Chuwa, Johari Shani (Uhuru Digital) na Abel Ngapemba ambaye ni Afisa Habari Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza.
Waandishi waliofariki katika ajali hiyo walikuwa katika ziara ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Gabriel kuelekea Wilaya ya Ukerewe kupitia Bunda.
Ziara hiyo iliyolenga kukagua na kupokea miradi ya madarasa imesitishwa kwa muda.
Ajali hiyo iliyogharimu watu muhimu katika tasnia ya habari imetokea ikiwa zimezipita wiki tano tangu itokea ajali kama hiyo ilihusisha wanahabari waliokuwa kwenye msafara wa Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Brigedia Jenerali Marco Gaguti uliokuwa unaelekea wilayani Newala kutekeleza mradi wa mapambano ya Uviko-19.
Katika ajali hiyo, gari lililowabeba waandishi wa habari liligongana nagari lingine na kujeruhi waandishi wa habari wanne
Pia ajali nyingine kubwa iliyogharimu maisha ya wanahabri ndani ya kipindi cha miaka sita iliyopita ni ile iliyotokea eneo la Mwika mkoani Kilimanjaro mwaka 2017 ambapo watu sita wakiwemo waandishi wa habari wawili walipoteza maisha baada ya gari lao kugongwa na gari nyingine aina ya Fuso.
Latest
