Rais Samia ataka makatibu mahsusi, masijala kutunza siri Tanzania
- Watakiwa kuzingatia kiapo cha kutunza siri, weledi na kufanya kazi kwa mipaka
- Rais asema waige muundo wa CWT utakaowasaidia kutatua changamoto zao
Dar es Salaam. Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amewataka makatibu mahsusi na watunza kumbukumbu nchini kufanya kazi kwa weledi huku akiwaonya watakaovunja kiapo chao kuwa atakutana nao “mbele kwa mbele”.
Makatibu mahsusi na watunza kumbukumbu serikalini na sekta binafsi ni miongoni mwa watumishi muhimu ambao wanaohusika katika utunzaji wa taarifa nyeti za taasisi zao na kuwahudumia kwa karibu zaidi viongozi.
Watumishi hao kwa mara ya kwanza wamekula kiapo cha kutunza siri visiwani Zanzibar ikiwa ni moja ya jitihada za kuongeza utunzaji wa nyaraka za Serikali au za taasisi binafsi kutotolewa nje ya mamlaka husika bila utaratibu maalumu.
Katika hafla ya kufunga Mkutano wa Kitaaluma wa Chama cha Makatibu Mahsusi Tanzania (TAPSEA) pamoja na Menejimenti ya Watunza Kumbukumbu na Nyaraka (TRAMPA) leo Mei 27, 2023, Rais amewaambia washiriki hao kuwa wanatakiwa kuzingatia weledi, maadili na kiapo chao cha uaminifu.
“Inafurashisha kuona mnakamilisha mafunzo yenu kwa kula kiapo cha uaminifu, imeleta maana kubwa sana, mmekula kiapo mkishuhudiwa na Rais, kati yenu mtu akienda kinyume na kiapo chake atachukuliwa hatua za kisheria, naomba mkaishi viapo vyenu,” amesema Rais Samia mjini Fumba visiwani Zanzibar.
Soma zaidi
-
Yafahamu matunda yanayoweza kutibu na kukupa kinga ya maradhi
-
Jinsi ya kuhariri na kuficha meseji zako WhatsApp
-
Namna ya kuepuka kupokea barua pepe usizozihitaji
Hii ni mara ya pili ndani ya mwaka mmoja kwa kiongozi huyo wa juu kutumia mkutano kama huo kuwakumbusha washiriki wa mkutano huo umuhimu wa kutunza nyaraka na siri za taasisi wanazofanyia kazi kwani ndio moyo wa Serikali.
Washiriki zaidi ya 6,000 wa TAPSEA na TRAMPA wameapa kiapo cha kutunza siri za taasisi zao leo mbele ya Wakili wa Serikali Faraji Nguka ambapo wameshuhudiwa na Rais Samia.
Licha ya moja ya taasisi hizo, Tapsea kutimiza miaka 15 tangu kuanzishwa kwake bado inakabiriwa na udhaifu katika uendelezaji miradi na matatizo ya kimuundo.
Igeni muundo wa CWT
Ili kuzifanyia maboresho taasisi hizo, Rais Samia amezitaka taasisi hizo mbili kuboresha miundo ya uendeshaji kutokana na ongezeko la wanachama.
Katika ushauri wake, amesema zinapaswa kujifunza namna Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) kinavyojiendesha jambo litakalowasaidia kutatua baadhi ya changamoto zao wenyewe ikiwemo kuanzisha mifuko inayotambuliwa kisheria.
Kwa mujibu wa Ikulu Rais Samia amewahi kuwa Karani wa Masjara wa Serikali ya Zanzibar kati ya mwaka 1977 hadi 1983 alipopandishwa cheo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye viwanja vya Fumba kwa ajili ya kushiriki Kikao maalum cha Makatibu Mahsusi pamoja na Watunza Kumbukumbu na Nyaraka kabla ya kufunga Mkutano wa Kitaaluma wa Chama cha Makatibu Mahsusi Tanzania (TAPSEA) pic.twitter.com/gjFjLvFLr0
— ikulu_Tanzania (@ikulumawasliano) May 27, 2023
Latest