Rais Magufuli, Watanzania wawalilia waliofariki katika mlipuko wa lori la mafuta Morogoro
- Ajali hiyo imetokea Msamvu, Morogoro asubuhi ya leo kusababisha vifo zaidi ya 60 na majeruhi zaidi ya 70.
- Aagiza majeruhi wote wapatiwe matibabu haraka ili kuokoa maisha yao.
- Makamu wa Rais, Watanzania waomboleza watu waliofariki katika ajali hiyo.
Dar es Salaam. Rais John Magufuli ameungana na Watanzania kuomboleza vifo vya watu zaidi ya 60 waliopoteza maisha baada ya lori la mafuta kulipuka leo asubuhi katika eneo la Msamvu mkoani Morogoro na kuagiza majeruhi wote wapatiwe matibabu haraka ili kuokoa maisha yao.
Ajali hiyo pia imesababisha majeruhi zaidi ya 70 ambao waliungua moto sehemu mbalimbali za miili yao.
Kwa mujibu wa taarifa ya Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu inaeleza kuwa ajali hiyo imetokea leo (Agosti 10) saa 2:00 asubuhi ambapo lori hilo lililokuwa likitoka Dar es Salaam lilipinduka jirani na kituo cha mabasi cha Msamvu baada ya dereva wa lori kumkwepa mwendesha pikipiki na kisha mafuta yaliyokuwa yakimwagika kushika moto na kuunguza watu waliokuwa wanayachota.
Rais Magufuli ametoa pole kwa familia, ndugu, marafiki na wote waliopoteza jamaa zao katika ajali hiyo na pia amewaombea majeruhi wapone haraka.
“Nimeumia sana kusikia idadi kubwa ya Watanzania wenzetu waliopoteza maisha katika ajali hii, natoa pole kwa wote walioguswa na vifo hivi hasa familia za Marehemu wote, nawaombea Marehemu wapumzike mahali pema peponi na majeruhi wote wapone haraka” amesema Rais Magufuli na kumuagiza Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dk Kebwe Steven Kebwe kufikisha salamu zake za pole kwa familia na wote walioguswa na vifo hivyo.
Soma zaidi: Zaidi ya watu 57 wafariki dunia baada ya lori la mafuta kuwaka moto Morogoro
Dk Magufuli ameagiza Wizara zote zinazohusika kushughulikia ajali hiyo na ametaka Hospitali ya Mkoa wa Morogoro kwa kushirikiana na Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kuhakikisha majeruhi wote wanapatiwa matibabu ili kuokoa Maisha yao.
Aidha, ameelezea kusikitishwa kwake na vitendo vya watu kuvamia magari yanayopata ajali kwa lengo la kujipatia bidhaa mbalimbali zilizobebwa na magari hayo na ametaka vitendo hivyo vikome.
“Baadhi ya magari haya yanabeba mafuta ambayo ni hatari kama ilivyotokea Morogoro, yapo magari yanabeba kemikali za sumu, yapo magari yanabeba milipuko nakadhalika, nawaomba sana tuache tabia hii,” amesema Magufuli.
Askari na watu wakizima moto uliotokana na mlipuko wa lori la mafuta mkoani Morogoro na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 60. Picha|Mtandao.
Viongozi na wananchi wa kada mbalimbali wameungana na Rais kuomboleza vifo vya watu waliopoteza maisha huku wengine wakitaka wananchi kuelimishwa kuhusu tahadhari ya malori yanayobeba mafuta.
Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan amesema amepokea kwa majonzi taarifa ya ajali ya moto mkoani Morogoro iliyopelekea vifo na majeruhi kwa ndugu zetu Watanzania.
“Naungana na Watanzania wenzangu kutoa pole na kuwaombea Marehemu wote wapumzike mahali pema peponi. Pia tunawaombea majeruhi wote wapate aheuni mapema,” ameandika Mama Samia katika ukurasa wake wa Twitter.
Nimepokea kwa majonzi taarifa ya ajali ya moto mkoani Morogoro iliyopelekea vifo na majeruhi kwa ndugu zetu Watanzania.
Naungana na Watanzania wenzangu kutoa pole na kuwaombea Marehemu wote wapumzike mahali pema peponi. Pia tunawaombea majeruhi wote wapate aheuni mapema.
— Samia Suluhu (@SuluhuSamia) August 10, 2019