Kinachofuata baada ya Nchimbi kujiuzulu
- Kwa mujibu wa katiba ya Tanzania, Ibara ya 50(4), inasema iwapo nafasi ya Makamu wa Rais itakuwa wazi kwa sababu ya kifo ama kujiuzulu, Rais anatakiwa kumteua mtu mwingine kushika hiyo ndani ya siku 14.
Dar es Salaam. Makamu wa Rais wa Tanzania, Dk Emmanuel Nchimbi ametangaza kujiuzulu na kuachia madaraka kwenye nafasi hiyo, kuanzia September 4 mwaka huu.
Dk Nchimbi alimuandikia barua ya kujizulu Rais Samia hapo jana Agosti 25, 2026 akisema kwamba amejiridhisha pasina shaka kuwa Rais Samia anatamani mabadiliko kwenye nafasi hiyo na saa chache baadaye Rais Samia aliridhia ombi hilo.
Unachotakiwa kufahamu ni kwamba kujiuzulu kutoka katika cheo cha Makamu wa Rais ni kumeruhusiwa kikatiba.
Ibara ya 50(2)(c) ya Katiba ya Tanzania ya mwaka 1977 inaeleza kuwa Makamu wa Rais anaweza kuacha madaraka kwa njia ya kujiuzulu.
Lakini je, ni nini hufuata inapotokea Makamu wa Rais amejihudhuru na utaratibu gani hufuata ili kumpata makamu mpya?
Katiba ya Tanzania inaweka wazi utaratibu wa kujaza nafasi ya Makamu wa Rais iwapo nafasi hiyo itakuwa wazi kutokana na kujiuzulu au kifo.
Kwa mujibu wa katiba hiyo, Ibara ya 50(4), iwapo nafasi hiyo itakuwa wazi kwa sababu hizo, Rais anatakiwa kumteua mtu mwingine kushika nafasi ya Makamu wa Rais.
Uteuzi huo unatakiwa kufanywa haraka iwezekanavyo, na kwa hali yoyote ndani ya siku 14 tangu Makamu wa Rais kuacha madaraka.
Hata hivyo, Mtu anayeteuliwa na Rais anatakiwa kuidhinishwa na Bunge kwa kura ya wengi wa wabunge kabla ya kuapishwa rasmi nakuanza kutekeleza majukumu yake.
Kwa mujibu, Wakili Peter Majanjara kutoka Chika Attorneys anasema licha ya Rais Samia kuridhia ombi la Nchimbi kujiudhuru, bado Dk Nchimbi anasalia kuwa makamu wa Rais hadi pale atakapo ng’atuka rasmi Septemba 4.
Hii ina maana kuwa siku 14 zinazotoa nafasi ya kufanyika kwa mchakato wa kumpata Makamu wa Rais Mpya zitaanza kuhesabiwa kuanzia Septemba 4 siku ambayo Nchimbi ataachia madaraka rasmi.
Hata hivyo, Majanjara anaeleza kuwa katiba haijaweka wazi kwamba ni nini kitatokea iwapo siku hizo 14 zitapita.
Je, unahisi ni nani anakwenda kurithi nafasi ya Nchimbi?