Mkaa, samani vyachangia kushusha mfumuko wa bei Tanzania
- Umepungua hadi asilimia 3 kutoka asilimia 3.1 iliyorekodiwa Mwezi Julai.
- Vifaa vya ujenzi, mkaa, na samani vyasaidia mfumuko wa bei kushuka.
Dar es Salaam. Kasi ya mfumuko wa bei za bidhaa na huduma nchini Tanzania kwa mwaka unaoishia Julai 2024 imepungua kidogo hadi asilimia 3 kutoka asilimia 3.1 iliyorekodiwa mwaka unaoishia Juni 2024 ikichochewa zaidi na kupungua kwa mfumuko wa bei za bidhaa zisizo za chakula.
Hii inamaanisha kuwa kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma kwa mwaka ulioishia mwezi Julai, 2024 imepungua ikilinganishwa na kasi iliyokuwepo kwa mwaka ulioishia mwezi Juni 2024.
Mfumuko wa bei wa Taifa hupima kiwango cha kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma zote zinazotumiwa na kaya binafsi nchini.
Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) leo Agosti 9, 2024 imebainisha kuwa kupungua kwa kasi ya mfumuko wa bei kwa mwaka ulioishia Julai 2024 kumechangiwa na kupungua kwa mfumuko wa bei wa baadhi ya bidhaa zisizo za chakula.
Tangu mwaka 2024 uanze kasi ya mfumuko wa bei imekuwa kati ya asilimia 3.0 na 3.1, kiwango ambacho kipo ndani ya wigo wa Serikali wa kuwa na mfumuko wa bei kati ya asilimia 3.0 na asilimia 5.0.
Baadhi ya bidhaa zisizo za chakula zilizochangia kupungua kwa mfumuko wa bei kwa mwaka ulioishia mwezi Julai 2024 ni vitambaa vya kushona nguo kutoka asilimia 1.6 hadi 1.3; bidhaa kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa jengo (kutoka asilimia 3.1 hadi 1.6) na mkaa ambao mfumuko wa bei ulishuka kutoka asilimia 29.3 hadi 28.4.

Bidhaa nyingine zisizo za vyakula zilizochangia kupungua kwa mfumuko wa bei ni samani za nyumbani kutoka asilimia 4.7 hadi 4.5.
Hata hivyo, taarifa ya NBS imebainisha kuwa mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa mwaka ulioishia mwezi Julai, 2024 umeongezeka kidogo hadi asilimia 1.0 kutoka asilimia 0.9 kwa mwaka ulioishia mwezi Julai, 2024.
Aidha, mfumuko wa bei ambao haujumuishi bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa mwaka ulioishia mwezi Julai, 2024 umepungua hadi asilimia 3.8 kutoka asilimia 4.0 kwa mwaka ulioishia mwezi Juni, 2024.
Mfumuko wapanda Uganda, Kenya ahueni
Kwa mujibu wa NBS nchini Uganda, mfumuko wa bei kwa mwaka ulioishia mwezi Julai, 2024 umeongezeka hadi asilimia 4.0 kutoka asilimia 3.9 kwa mwaka ulioishia mwezi Juni, 2024.
Kwa upande wa Kenya, mfumuko wa bei kwa mwaka ulioishia mwezi Julai, 2024 umepungua hadi asilimia 4.3 kutoka asilimia 4.6 kwa mwaka ulioishia mwezi Juni, 2024.
Kenya kwa muda wa miezi miwili sasa bado haijawa na utulivu wa kuridhisha kutokana na maandamano yanayoendelea yaliyolenga kupinga muswada mpya wa Sheria ya Fedha, kupanda kwa gharama za maisha pamoja na kuishinikiza Serikali ya Rais William Ruto kuondoka madarakani.
Latest