Mikopo kwa sekta binafsi yapungua Tanzania
- Imepungua hadi wastani wa asilimia 8.6 katika mwaka ulioishia Machi 2020 ikilinganishwa na asilimia 9.6 katika kipindi kama hicho mwaka 2019.
- Sehemu kubwa ya mikopo hiyo bado inaelekezwa katika shughuli za watu binafsi na biashara.
Dar es Salaam. Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imesema mikopo kwa sekta binafsi imepungua kidogo ndani ya kipindi cha mwaka mmoja uliopita, licha ya sehemu kubwa ya mikopo hiyo kuelekezwa katika shughuli za watu binafsi na biashara.
Ripoti ya Tathmini ya Uchumi ya mwezi Aprili 2020 (Economic Monthly Review) iliyotolewa na BoT hivi karibuni inaeleza kuwa mikopo kwa sekta binafsi imepungua hadi wastani wa asilimia 8.6 katika mwaka ulioishia Machi 2020 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 9.6 katika kipindi kama hicho mwaka 2019.
“Hii inaashiria kuwa kwa sehemu kuna pesa za kutosha za kukopesha kutokana na hatua mbalimbali zinachukuliwa na Serikali kuimarisha sera za fedha,” inaeleza ripoti hiyo.
Ripoti hiyo inaeleza kuwa sehemu kubwa ya mikopo kwa sekta binafsi imeendelea kuelekezwa kwa watu binafsi ambao walipata wastani wa asilimia 30.2 ya mikopo yote ikifuatiwa na shughuli za biashara zilizokuwa na wastani wa asilimia 17.7.
Soma zaidi:
- Serikali yaanika bajeti ya mwaka 2019/2020
- Serikali yasema ongezeko la bajeti ya kilimo litategemea mahitaji ya kibajeti ya sekta nyingine
- Kasi ya ukopeshaji sekta binafsi yapaa mara tatu
Mikopo inayoelekezwa katika shughuli zote kubwa za uchumi imeendelea kuongezeka, isipokuwa kwa shughuli za hoteli na migahawa, madini na uzalishaji viwandani.
Hata wakati mikopo kwa sekta binafsi ikipungua, kiwango vya riba kinachotozwa na benki za biashara nacho kimeshuka.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, riba iliyotozwa kwenye mikopo iliyotolewa na benki ilikuwa ni wastani wa asilimia 15.83 mwezi Machi 2020 ikishuka kutoka wastani wa asilimia 17.59 katika kipindi kama hicho 2019.
Wiki hii BoT imetangaza hatua mbalimbali kupunguza makali ikiwemo kuziruhusu benki kujadiliana na wakopaji wao juu ya urejeshaji mikopo ili kupunguza maumivu wakati huu wa mlipuko wa Corona uliosababishwa kuyumba kwa shughuli za uchumi.
Latest
