Mikakati ya Tanzania kujikwamua na uhaba wa dola
- Ni pamoja na uuzaji dhahabu pamoja na kukopa kutoka kwa mataifa ya nje.
- Mikakati hiyo itaiwezesha Serikali kupata akiba ya Dola za Marekani.
Dares Salaam. Serikali ya Tanzania imeanza kutekeleza mikakati ya kuongeza upatikanaji wa Dola nchini, ikiwemo kununua dhahabu ili kuwezesha upatikanaji wa huduma zinazotegemea fedha hiyo.
Uhaba wa Dola ya Marekani unaoyakabili mataifa mbalimbali duniani ikiwemo Tanzania umesababisha mfumuko wa bei ya baadhi ya bidhaa muhimu kama vile mafuta, saruji pamoja na huduma za usafiri.
Msemaji Mkuu wa Serikali Gerson msigwa, aliyekuwa akizungumza na waandishi wa habari leo Agosti 26, 2023 Jijini Dar es Salaam, amesema Serikali ya Tanzania kupitia Benki Kuu ya Tanzania (BOT) imeshanunua kilogramu 400 katika kipindi cha mwezi Mei hadi Julai 2023.
“Kupitia Benki kuu ya Tanzania pale tunanunua dhahabu maana yake ukienda kuiuza unapata Dola (za Marekani)…tumeanza tangu mwezi wa tano mwaka huu, kati ya mwezi wa tano na wa saba tumenunua karibu kilo 400 za dhahabu,” amesema Msigwa.
Kwa mujibu wa tovuti ya ‘Live price of Gold’ inayotoa viwango vya kubadilisha dhahabu, kilo moja ya dhahabu nchini Tanzania leo Agosti 26, 2023 imeuzwa kwa Sh153.7 milioni sawa na Dola 61,580.31. za Marekani.
Hiyo ni sawa na kusema kama Tanzania ikiamua kuuza Dola hizo inaweza kujiingizia Sh61.4 bilioni sawa na Dola 24.6 milioni, ambazo zinaweza kupunguza uhitaji wa fedha hiyo ya kigeni.
Soma zaidi
-
Hapana: Marekani haibadilishi noti za fedha zake
-
Kutana na mbunifu wa majiko yanayotumia mawe Tanzania
Mikakati mingine
Sambamba na hayo Serikali imejipanga kutafuta mikopo kutoka kwa mataifa ya nje ili kuongeza upatikanaji wa dola, pamoja na kuwasapoti wafanyabiashara kuzalisha zaidi na kufanya mabadilishano ya fedha (swapping) na wafanyabiashara waliopo nchini.
“Wataalamu wa uchumi kuna kitu wanaita ‘swapping’ Serikali inawezesha wafanyabiashara tunawapatia shilingi wao wanatupatia Dola (za Marekani), halafu siku tukiwa na Dola nyingi wanaturudishia shilingi zetu,” amefafanua Msigwa.
Pia Serikali itatoa dhamana kwa bidhaa zinazouzwa nje (Export Credit Guarantee Scheme) ikiwa ni mkakati mwingine unaopangwa kutekelezwa ambapo utawezesha upatikanaji wa Dola ya Marekani yaani mabenki yatawapa mikopo wafanyabiashara na wao watachangia asilimia 50.

Ili kukabiliana na uhaba wa Dola ya Marekani unaoendelea katika nchi nyingi Duniani Gerson Msigwa amewaambia wanahabari kuwa kuongeza uzalishaji wa bidhaa za kilimo kunaweza kuwa suluhu ya muda mrefu ya uhaba wa Dola.Picha|Global.
Benki kuuza dola kwa bei nafuu
Benki Kuu ya Tanzania (BOT) ina utaratibu wa kuuza Dola kwa mabenki kwa bei ya jumla, ambapo kutokana na uhaba wa fedha hiyo benki hiyo itauza Dola kwa bei nafuu zaidi ili kuwezesha mabenki kushusha viwango vya kubadilishia dola kwa wananchi.
Jana Agosti 25, 2023, BOT imewauzia mabenki Dola za Marekani milioni 20 ili kuwawezesha kutoa huduma kwa wanachi wanaotaka kutumia fedha hizo kununua huduma na bidhaa mbalimbali.
Hata hivyo, Msigwa amesema utaratibu wa kuuza dola kwa bei nafuu ni kwa ajili ya mabenki tu, mwananchi mmoja mmoja hatahusika na punguzo la thamani ya dola inayotolewa na BOT.
Aidha mkakati mwingine uliowekwa na Serikali ni kuendelea kutoa leseni kwa wanaotaka kufungua maduka ya kubadilishia fedha, ambapo zaidi ya 80 zimetolewa wakati wafanyabiashara waliokuwa wamefungiwa awali na sasa wana vigezo wameshafunguliwa.
Mpaka sasa Serikalii imerudisha zaidi ya Sh9 bilioni kwa wafanyabiashara ambao fedha zao zilishikiliwa kimakosa.
Latest
