Mgonjwa wa kwanza afariki dunia kwa corona Tanzania
- Amefariki leo asubuhi katika kituo cha matibabu cha wagonjwa wa COVID-19 kilichopo Mloganzila jijini Dar es Salaam.
- Marehemu ni Mtanzania, mwanaume mwenye umri wa miaka 49 ambaye pia alikuwa akisumbuliwa na maradhi mengine.
- Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu awataka Watanzania kuendelea kuchukua tahadhari.
Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imetangaza kifo cha kwanza cha mgonjwa wa virusi vya Corona kilichotokea alfajiri ya leo ( Machi 31, 2020) jijini Dar es Salaam.
Taarifa iliyotolewa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu leo inaeleza kuwa mgonjwa huyo amefariki katika kituo cha matibabu cha wagonjwa wa COVID-19 kilichopo Mloganzila jijini Dar es Salaam.
Amesema marehemu huyo ni Mtanzania, mwanaume mwenye umri wa miaka 49 ambaye pia alikuwa akisumbuliwa na maradhi mengine.
Hadi kufikia leo, Tanzania imethibitisha kuwa na wagonjwa 19 wa virusi hivyo vinavyosambaa kwa kasi duniani ambapo mgonjwa mmoja kati ya hao tayari amepona.
Mkoa wa Dar es Salaam ndiyo unaongoza kuwa na wagonjwa wengi wa Corona wanaofikia 11 ukifuatiwa na visiwa vya Zanzibar (5), Arusha (2) na mmoja alithibitishwa katika mkoa wa Kagera.
“Kazi ya kufuatilia watu waliokutana na wagonjwa hawa inaendelea (contact tracing). Aidha tunawataka wananchi wote waendelee kuchukua tahadhari kujikinga na ugonjwa huu,” alisema Ummy jana wakati akitangaza wagonjwa wengine watano wa Corona.
Zinazohusiana
Tahadhari ambazo zinatakiwa kuchukuliwa ni pamoja na kunawa mikono mara kwa mara, kutokugusa macho, pua au mdomo, kutumia tishu wakati wa kukohoa na kuepuka mikusanyiko ya watu isiyo ya lazima.
Mpaka sasa ni nchi nne za Afrika Mashariki za Tanzania, Kenya, Uganda na Rwanda ndiyo zimethibitisha kuwa na wagonjwa wa vurusi hivyo na vifo vya watu wawili wa ugonjwa vilivyotokea Kenya na Tanzania.
Latest