Rais Samia adokeza vipaumbele Dira ya Maendeleo 2050
- Ni pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi ili kuongeza upatikanaji wa ajira kwa wananchi.
Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imebainisha baadhi ya maeneo yatakayopewa kipaumbele katika maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050 ikiwemo kuchochea ukuaji wa uchumi kwenye maeneo ya uzalishaji yanayowagusa wananchi.
Rais Samia Suluhu Hassan, amewaeleza washiriki wa hafla ya maadhimisho ya miaka 62 ya uhuru wa Tanzania Bara jijini Dodoma leo Disemba 9, 2023, vipaumbele hivyo vimetokana na ripoti ya tathmini ya utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya mwaka 2025 itakayomalizika miaka miwili ijayo.
“Maeneo yatakayopewa kipaumbele ni kama ifuatavyo ukuaji wa uchumi kufugamanishwa na sekta za uzalishaji kama kilimo na nyingine za uzalishaji,” amesema Rais Samia.
Amesema dira hiyo iwe na kipaumbele cha kuchochea ukuaji wa uchumi katika maeneo ya uzalishaji yanayomgusa mwananchi mmoja mmoja, jambo litakalochochea upatikanaji wa ajira.

Baadhi ya wahudhuriaji wa maadhimisho ya miaka 62 ya uhuru wa Tanzania Bara na Mkutano wa Kwanza wa Kitaifa wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.Picha|Ikulu
Kitabu cha hali ya uchumi kwa mwaka 2022 kilichotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kinabainisha kuwa hadi kufikia mwaka 2020/2021 Tanzania ilikuwa na asilimia 12.9 ya vijana wenye umri kuanzia miaka 15 hadi 35 wasiokuwa na ajira. Hii ina maana kuwa vijana 13 kati ya 100 wenye umri huo hawakuwa na ajira inayowasaidia kuingiza kipato.
Vijana wenye umri wa miaka 15 mpaka 35, kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi kwa mwaka 2022, walikuwa milioni 20.6. Kwa idadi hiyo, ina maana kuwa zaidi ya vijana milioni 2.6 wenye umri wa miaka 15 hadi 35 hawana ajira nchini ukiachana na wale wenye umri huo ambao bado wapo masomoni.
Rais Samia amebainisha pia kuwa dira mpya ya mwaka 2050 itaimarisha uendeshaji wa mashirika ya Serikali pamoja na yale sekta binafsi kutoka ndani na nje ya nchi huku ikifanya tathmini na ufuatiliaji katika utekelezaji wa mipango yote ya nchi.
Kipaumbele cha tathmini na ufuatiliaji wa mipango ya nchi kimewekwa chini ya tume ya mipango ambayo muswada wake umeidhinishwa na Bunge hivi karibuni. Tume hiyo inatarajiwa kusaidia utekelezaji wa shughuli nyingine za maendeleo nchini.
“Uwepo wa taasisi ya tume ya mipango utakwenda kuondosha changamoto hiyo…si katika utekelezaji wa dira ijayo tu bali katika utekelezaji wa mipango yote ya maendeleo ya nchi yetu,” amesema Rais Samia.
Soma zaidi:Jinsi Tanzania inavyoweza kuongeza upatikanaji wa haki za binadamu
Serikali pia kupitia dira ya mwaka 2050 ina mpango wa kuyaimarisha mashirika ya umma na sekta binafsi ili ziweze kujiendesha kwa faida na kukuza uchumi wa taifa
“Dira iweke uelekeo wa uwekezaji na usimamizi wa maboresho ya kiutendaji wa mashirika ya Serikali ili yaongeze ufanisi katika uendeshaji na yaweze kuhimili ushindani wa kikanda na kimataifa…sekta binafsi Serikali tupo tayari kuwaimarisha na muwe tayari kuimarika,” amesema Rais Samia.
Itakumbukwa kuwa Agosti 19, 2023 jijini Arusha, Rais Samia aliyataka mashirika ya umma kujitegemea na kujiendesha kwa faida ili kupunguza mzigo kwa Serikali.
Pia alitoa mapendekezo ya kuanzishwa kwa mifuko utakaosimsmia mashirika hayo ili kuondoa utegemezi kutoka mfuko mkuu wa Serikali.