Mama Samia Suluhu: Mimi ndiye Rais wa Tanzania
- Amesema yeye ni Rais wa Tanzania mwenye maumbile ya mwanamke.
- Awatolea uvivu wanaohofia uwezo wake katika kuongoza.
Dar es Salaam. Rais wa sita wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amesema kwa wale ambao wana mashaka kuwa anaweza kuwa rais, wafahamu kuwa yeye ni Rais mwenye maumbile ya mwanamke.
Rais Samia, aliyekuwa akizungumza leo Machi 22, 2021 jijini Dodoma wakati wa kumuaga kitaifa Hayati Rais John Magufuli, amesema Watanzania hawapaswi kuwa na mashaka yoyote kuhusu uwezo wake wa kuongoza nchi.
“Kwa wale ambao wana mashaka kuwa mwanamke huyu ataweza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nataka niwaambie aliyesimama hapa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye maumbile yake ni mwanamke,”- amesema Samia huku akishangiliwa na umati wa watu waliojitokeza uwanja wa Jamhuri kumuaga hayati Magufuli.
Soma zaidi:
- Rasmi: Samia Suluhu Hassan aapishwa kuwa Rais wa Tanzania
- Huyu ndiye Samia Suluhu Hassan, Rais mwanamke wa kwanza Tanzania
Mama Samia, ambaye aliapishwa Machi 19 mwaka huu kuwa Rais mpya wa Tanzania baada ya kifo cha Dk Magufuli Machi 17 mwaka huu, amesema Serikali yake itaendeleza mazuri yote aliyoasisi Rais Magufuli kwa sababu aliwapika vizuri na viongozi wote wako imara kutekeleza majukumu yao.
“Tunapokwenda kumpumzisha, tunaweza kusema bila kigugumizi tuko tayari kuendeleza kazi yake nzuri kwa nguvu, kasi na hali ile ile,” amesema.
Rais Samia amesema kuwa yeye na Rais wa Zanzibar Hussein Mwinyi wataendeleza alipoishia hayati Rais Magufuli na kuifikisha Tanzania mahali ambapo alitamani ifike.
Viongozi mbalimbali wakiwemo wa kitaifa na kimataifa wamejitokeza jijini Dodoma kutoa salamu za mwisho kwa mwili wa Dk Magufuli ambaye atazikwa Chato mkoani Geita Machi 26 mwaka huu.