Majaliwa awapa kibarua kigumu maafisa habari serikalini
- Awataka wahakikishe wananchi wanapata elimu na taarifa sahihi.
Dar es Salaam. Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amewataka maafisa habari, mawasiliano na uhusiano serikalini waongeze ubunifu wa kutoa taarifa sahihi kwa kusukuma ajenda za Serikali kwa umma na si kusubiri kazi zifanywe na waandishi wa habari wengine.
Majaliwa aliyekuwa akizungumza leo Machi 27, 2023 wakati akifungua kikao kazi cha 18 cha Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano Serikalini kilichoanza leo katika Kituo Cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam amesema pia wana wajibu wa kutoa taarifa kwa wananchi.
“Mnapofanya kazi ongezeni ubunifu wa kusukuma ajenda za Serikali kwa umma na msisubiri kazi zifanywe na wanahabari wengine. Hakikisheni kila mwananchi anapata elimu na taarifa sahihi kuhusu faida na umuhimu wa miradi na mipango au shughuli zinazotekelezwa na Serikali,” amesema Majaliwa.
Waziri Mkuu aliyekuwa akimwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan amesema maafisa hao wana wajibu wa kuhakikisha kuwa yale yote yanayopangwa na kutekelezwa na Serikali yanafahamika kwa umma wa Watanzania kwa usahihi, kwa wakati na kwa tija.
Amesema wanapofanya mawasiliano hasa ya kimkakati, wahakikishe wanafahamu lengo la mawasiliano wanayotaka kufanya, faida na matarajio ya kutekeleza mawasiliano husika, nani mlengwa pamoja na kuchagua njia sahihi za mawasiliano.
“Nimeona nisisitize hayo kwa kutambua kuwa mafanikio ya Serikali hayana budi kufahamika kwa wananchi wote na ni wajibu wa kila taasisi kuhakikisha mawasiliano hayo yanakuwa ya kimkakati ili yaweze kuleta tija na kufikia malengo yaliyokusudiwa,” amesisitiza Majaliwa.
Endeleeni kutoa elimu kwa umma kuhusu umuhimu wa kulinda mila, desturi na tamaduni za kitanzania hususan katika kipindi hiki tunachokabiliwa na wimbi kubwa la mmomonyoko wa maadili-Waziri Mkuu @KassimMajaliwa_
pic.twitter.com/P616hRDfFX— Ofisi ya Waziri Mkuu (@TZWaziriMkuu) March 27, 2023
Maagizo ni haya fuateni
Ili kuwawezesha maafisa hao kutekeleza majukumu yao, Waziri Mkuu amewaagiza makatibu wakuu wote, wakurugenzi wa halmashauri na taasisi zote za umma watenge bajeti ya kutosha kugharamia shughuli za utoaji wa taarifa pamoja na elimu kwa umma na kuhakikisha jukumu hilo linatekelezwa kwa tija na ufanisi uliokusudiwa.
Pia amewataka viongozi wa wizara na wakuu wa taasisi waweke kipaumbele cha kuwashirikisha maafisa habari kwenye vikao mbalimbali ikiwemo vikao vya menejimenti ili waweze kwenda na wakati na kupata ufahamu wa kutosha wa taasisi na mipango ya Serikali.
Mapema, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye amesema wizara hiyo ipo katika hatua za mwisho kukamilisha utayarishaji wa Mkakati wa Taifa wa Mawasiliano kwa Umma (The National Communications Strategy) ambao ukikamilika utaainisha na kufafanua utaratibu wa upatikanaji na usambazaji wa taarifa za Serikali kwa umma.
“Pamoja na mkakati huo, tuko kwenye hatua za mwisho za uandaaji wa Mkakati wa Mawasiliano Serikalini wakati wa Majanga (Risk Communication Strategy) na Mkakati wa Taifa wa Kujitangaza (National Branding Strategy).”
Mikakati hiyo ikikamilia itaweka misingi ya kusimamia usambazaji wa taarifa zenye maudhui ya ajenda za kitaifa, kuboresha mbinu na teknolojia ya ukusanyaji, uchakataji na usambazaji wa taarifa za Serikali kwa wananchi.
Kikao kazi hicho kinachotarajiwa kumalizika Machi 31, 2023 kinahudhuriwa na washiriki zaidi ya 500 ambao ni maafisa habari, mawasiliano na uhusiano serikalini kutoka Tanzania Bara na Zanzibar kwenye wizara mbalimbali, taasisi za umma, halmashauri na idara zinazojitegemea.