Diaspora watakiwa ‘kuvaa ubalozi’ fursa Tanzania

October 29, 2022 6:19 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Waziri Mkuu awataka kushawishi na kuvutia uwekezaji nchini Tanzania.
  • Awataka kujenga taswira nzuri ya Tanzania huko waliko.

Dar es Salaam. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewataka Watanzania wanaoishi ughaibuni kuwa mabalozi wazuri kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za nchi wanazoishi ili kujenga taswira nzuri ya Tanzania huko waliko.

Majaliwa aliyekuwa akizungumza na Watanzania waishio Jamhuri ya Korea jana (Oktoba 28, 2022) pia amewataka Watanzania hao watumie fursa walizonazo kushawishi na kuvutia uwekezaji nchini Tanzania.

 “Tumieni ushawishi na fursa mlizonazo kuwavutia wawekezaji na siku zote semeni mazuri na fursa za kiuchumi zilizopo Tanzania bila kusahau kuwasemea vizuri viongozi wakuu hasa dhamira nzuri ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ya kuliletea maendeleo Taifa,” amesema Rais Samia. 

Majaliwa amewataka wajenge utamaduni wa  wa kutumia lugha ya Kiswahili kama fursa ya kiuchumi kwani nchi nyingi zinahitaji walimu, waandishi, watangazaji na wakalimani wa lugha hiyo ya Taifa.

Amewahakikishia kuwa Tanzania ipo salama na Rais Samia anafanya juhudi kubwa kuhakikisha kwamba maisha ya Watanzania  yanaimarika kwa kuendelea kusogeza karibu huduma mbalimbali za kijamii ikiwemo maji, umeme na elimu.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Watanzania wanaoishi nchini Korea John Bakunda ameipongeza Serikali kwa utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo pamoja na kuendelea kuimarisha diplomasia ya kiuchumi na mataifa mbalimbali duniani.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW