Ripoti mauaji Tanga, Mtwara yatua kwa Majaliwa, atoa mwelekeo
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amepokea taarifa ya kamati maalum aliyoiunda kwa ajili ya kuchunguza mauaji katika Mkoa wa Mtwara na Wilaya ya Kilindi, Tanga. Picha\ Ofisi ya Waziri Mkuu.
- Kamati iliyoundwa yakamilisha kazi na kumkabdhi Waziri Mkuu.
- Itapelekwa kwa Rais Samia kwa hatua zaidi.
- Mauaji hayo ni ya mfanyabiashara wa madini Mtwara na sita wa Tanga.
Dar es Salaam. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema ripoti ya mauaji yaliyotokea hivi karibuni katika mikoa ya Mtwara na Tanga tayari imekamilika na ataiwasilisha kwa Rais Samia Suluhu Hassan ili hatua zichukuliwe dhidi ya wahusika.
Majaliwa amepokea taarifa ya kamati maalum aliyoiunda kwa ajili ya kuchunguza mauaji ya mfanyabiashara wa madini katika Mkoa wa Mtwara yaliyodaiwa kufanywa na askari polisi na watu wengine sita waliouawa katika mapigano ya wakulima na wafugaji katika Wilaya ya Kilindi mkoani Tanga.
Waziri Mkuu aliyekuwa akizungumza baada ya kupokea taarifa hiyo Februari 26, 2022 jijini Dar es Salaam, ameipongeza kamati hiyo kwa kazi kubwa waliyoifanya na kwa umakini mkubwa.
“Taarifa hii imeeleza kila kitu bayana kabisa, na haya ndiyo matarajio ya Serikali yetu kwamba mtumishi yeyote ndani ya Serikali lazima awajibike kwa weledi, uaminifu na uadilifu mkubwa, kwa kufanya hivyo shughuli za kuwahudumia wananchi zitakwenda vizuri sana,” amesema Majaliwa.
Amesema kuwa baada ya kuipitia taarifa hiyo ataiwasilisha kwa Rais Samia ambaye ndiye aliyetoa maagizo ya kuundwa kwa kamati hiyo ya kuchunguza mauaji kwenye mikoa hiyo.
“Rais Samia anahitaji kuona matokeo, tena matokeo yasiyomuonea mtu yeyote, lakini matokeo yatakayomuwajibisha yeyote ambaye atagundulika kuhusika kutaka kuleta tafrani ndani ya nchi,” amesema Majaliwa bila kutaja waliohusika katika mauaji hayo na hatua zitakazochukuliwa dhidi yao.
Kamati hiyo ilianza kazi Februari 4, 2022 ilipaswa kukamilisha ripoti yake ndani ya siku 14, zilizoishia Februari 17, 2022. Lakini kutokana na ukubwa wa kazi na mahitaji ya kujiridhisha na baadhi ya masuala, kamati iliomba kuongezewa siku saba kuanzia Februari 17 hadi Februari 23, 2022.
Kamati hiyo iliundwa na Waziri Mkuu ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais Samia Suluhu Hassan alilolitoa Februari 4, 2022 Wilayani Magu, Mwanza akiwa njiani kuelekea Musoma, Mara kwenye maadhimisho ya miaka 45 ya CCM.
Katika mauaji ya Mtwara, askari nane wa Jeshi la Polisi ambapo mmoja alifariki dunia kwa madai ya kujinyonga wanatuhumiwa kutekeleza mauaji ya Mussa Hamisi (25), mkazi wa kijiji cha Ruponda Wilaya ya Nachingwea mkoani humo na kisha kumpora Sh70 milioni.
Imeelezwa kuwa tukio la mauaji ya kijana huyo walilitekeleza Januari 5, 2022 na mwili wa marehemu waliutupa katika kitongoji cha Majengo, Kijiji cha Hiari wilayani Mtwara.
Tukio la pili la Kilindi, watu sita waliuawa baada ya kutokea mapigano ya wakulima na wafugaji Januari 31, 2022.
Latest