Kula chakula hotelini, mgahawani hakuzidishi maambukizi ya Corona
- Miongozo ya kujikinga ikizingatiwa, maeneo hayo ni salama kupata huduma ya chakula.
- Watoa huduma za chakula wanatakiwa kuimarisha usafi maeneo yao.
Dar es Salaam. Ni matamanio ya nchi mbalimbali duniani kusikia maambukizi ya virusi vya ugonjwa wa Corona yakipungua kila siku.
Moja ya jitihada zinazofanyika kupunguza athari za ugonjwa huo ni kupambana na habari za uzushi zinazoweza kuleta athari kwa watu na jamii mbalimbali.
Moja ya uzushi unaosambaa kwenye mitandao ya kijamii ni kuwa watu wanaokwenda kupata huduma ya chakula kwenye migahawa au hotelini wanaongeza uwezekano wa kuambukizwa COVID-19.
Hata hivyo, habari hizo hazina ukweli wowote kwa sababu nchi nyingi zimelegeza masharti ya watu kukusanyika hasa katika shughuli za kijamii ikiwemo kupata chakula maeneo ya jumuiya.
Shirika la Afya Duniani (WHO) limeeleza kuwa kutembelea hotelini au mgahawani haiwezi kuwa sababu kuu ya kusambaza au kupata ugonjwa huo unaonezwa kwa njia ya kugusana.
“Pamoja na walaji kudhani kuna hatari ya kupata Corona kwenye maeneo ya huduma ya chakula, hakuna tafiti inayoeleza uhusiano kati ya huduma ya chakula na usambazaji wa virusi ya Corona,” imeeleza WHO katika mwongozo wake kwa wauzaji wa chakula duniani.
Zinazohusiana:
Shirika hilo ambalo ni msimamizi mkuu wa masuala ya afya duniani, limeeleza kuwa bado mtu anaweza kupata Corona akiwa katika maeneo yanayotoa huduma ya chakula, ikiwa hatazingatia miongozo ya kujikinga na ugonjwa huo.
Watoa huduma za chakula wanatakiwa kuzingatia miongozo ya usafi ili kuwaepusha watu na magonjwa ya mlipuko ikiwemo Corona.
Miongozo hiyo ni kuhakikisha umbali mita moja kutoka mteja mmoja na mwingine na watoa huduma kuvaa barakoa wakati wote wanapowahudumia watu hotelini.
Pia vifaa vya kunawia mikono, maji na vitakasa mikono vipatikane wakati wote wa huduma.
Kumbuka kuwa wataalam wanaendelea kufanya utafiti wa chanjo ya Corona ili kuudhibiti janga hilo ambalo ni tishio kwa mstakabali wa dunia. Endelea kuchukua tahadhari zinazopendekezwa na wahudumu wa afya
Latest