‘Famba’: Matunda, mboga mboga havisababishi Corona

November 25, 2020 10:23 am · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Hapana, virusi hivyo havienezwi kwa njia ya chakula.
  • Kinyume chake, unashauriwa kula kwa wingi matunda na mboga mboga. 

Dar es Salaam. Mapambano dhidi ya janga la Corona linaloitesa dunia bado yanaendelea licha ya kuwa idadi ya wagonjwa inaongezeka kila siku. 

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani(WHO), hadi kufikia jana Novemba 25, 2020 kumeripotiwa wagonjwa milioni 59.2 wa COVID-19 huku waliofariki kwa ugonjwa huo wakifikia milioni 1.4. 

Hata hivyo, mapambano ya COVID-19 siyo tu katika kutokomeza ugonjwa huo kwa kutafuta chanjo bali pia kukabiliana na habari za uzushi hasa zinazosambaa kasi kwenye mitandao ya kijamii.

Miongoni mwa uzushi ambao umekua ukivuma ni kuhusisha ulaji wa matunda na mboga mboga na maambukizi ya COVID-19 jambo ambalo ni uzushi au kwa lugha za vijana ni “famba”.  

Ukweli ni kuwa mtu hawezi kupata Corona kupitia ulaji wa vyakula hivyo, ambavyo kwa mujibu wa WHO vina virutubisho muhimu kwa ajili kujenga afya njema ya mwili. 

“Ni bahati mbaya kuwa watu hawawezi kupata COVID-19 kutoka kwenye vyakula,” imeeleza WHO katika tovuti yake


Zinahusiana:


Ugonjwa huo ni wa mfumo wa hewa (homa ya mapafu) na unaenezwa kwa njia ya kugusana au kugusa maji maji ya mgonjwa aliyeambukizwa baada ya kukohoa au kupiga chafya. 

WHO imewatoa watu hofu na kuwahimiza kula kwa wingi matunda na mboga mboga kwa sababu virusi vya ugonjwa huo havikai kwenye vyakula bali kwa binadamu na wanyama. 

“Osha matunda na mboga mboga kama unavyofanya katika mazingira mengine,” imesema WHO. 

Kumbuka kufuata miongozo ya afya inayotolewa katika eneo lako kuhusu kujikinga na ugonjwa huo ikiwemo kunawa mikono, kuvaa barakoa na kutumia tishu wakati wa kupiga chafya au kukohoa hasa kwa wale wanaosafiri kwenda kwneye nchi zenye maambukizi makubwa. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW