Kila baada ya dakika 1 watu 2 wanafariki kwa ajali za barabarani
- Hiyo ni sawa na takriban watu milioni 1.3 ambao hupoteza maisha kila mwaka.
- Sababu za kibinadamu huchangia kwa sehemu kubwa ajali hizo.
- WHO yawataka wadau kubuni njia mpya kumaliza ajali hizo.
Dar es Salaam. Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema kila baada ya dakika moja, watu wawili duniani hupoteza maisha kutokana na ajali za barabarani ambapo asilimia 90 ya wahanga hao wanatoka katika nchi zinazoendelea.
WHO katika chapisho lake lililotolewa Juni 28 hiyo ni sawa takriban watu milioni 1.3 ambao hupoteza maisha kila mwaka kutokana na ajali za barabarani.
Chapisho hilo linafafanua zaidi kuwa licha ya vifo hivyo, ajali za barabarani hujeruhi watu milioni 50 kwa mwaka, huku zikihusisha watembea kwa miguu na watumia baiskeli.
“Kifo kimoja kati ya vinne vinavyotokea kutokana na ajali za barabarani kinamuhusu mtembea kwa miguu au mwendesha baiskeli,” imeeleza WHO.
Ajali za barabarani nchini Tanzania zapungua
Mbali na takwimu za jumla za ajali za barabarani, Tanzania inachukua hatua mbalimbali kuhakikisha inapunguza ajali za barabarani ili kunusuru maisha ya wananchi.
Kwa mujibu wa ripoti ya Uhalifu na Makosa ya Usalama Barabarani za ya mwaka 2020 iliyotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) na Jeshi la Polisi, ajali za barabarani zimepungua kutoka 2,704 mwaka 2019 hadi ajali 1,714, zilizotokea mwaka 2020.
Ajali hizi zimepungua kwa asilimia 39.6, huku Zanzibar ikiwa na ajali 219 kwa mwaka 2020 ambapo kwa asilimia 0.5.
Zinazohusiana:
- Ajali, magonjwa ya kazini yanaua watu milioni 2 kila mwaka-WHO
- Watu 10 wafariki dunia ajali ya boti Pemba, polisi wakimsaka nahodha
Ajali za barabarani zilizotokea kwa mwaka 2020 nchini zimesababisha vifo vya watu 1,384 na majeruhi 2,362.
Ripoti hiyo inaeleza kuwa sababu za kibinadamu ndio chanzo kikubwa cha ajali za barabani ambapo asilimia 91 zinatokana na chanzo hiki, huku uzembe wa madereva na mwendo kasi vikitajwa kuchangia vifo hivyo.
Sababu nyingine iliyotajwa ni ubovu wa vyombo vya usafiri unaohusisha hitilafu za magari barabarani, sababu za kimazingira zikiwemo moto, vivuko vya reli na ubovu wa barabara.
UN yajipanga kupunguza nusu ya ajali za barabarani ifikapo 2030
WHO kwa kushirikiana na wadau wengine wa usalama barabarani, wameandaa mpango wa dunia wa karne ili kuchukua hatua za usalama barabarani, ambao utaweza kupunguza ajali za barabarani kwa asilimia 50 ifikapo mwaka 2030.
Mpango huo unatoa wito kwa serikali na wadau wote kuchukua njia mpya, ambayo itaokoa maisha na kuzuia majeraha, Ili kuzuia athari za kiuchumi za majanga yatokanayo na ajali yanayoweza kuzuilika.
Sambamba na hilo pia waimeitisha mkutano wenye kaulimbiu isemayo “Kuufikia mwaka 2030 kwa ajili ya usalama barabarani: kupata muongo wa utekelezaji na utimizaji”.
Mkutano huo una lengo la kukaribisha tamko la siasa au azimio litakalopitishwa na nchi wanachama wa UN, li kuimarisha usalama wa barabarani.
Latest