Kesi ya Lissu yaahirishwa hadi Msajili wa Mahakama atakapopanga ratiba
- Aweka pingamizi ushahidi wa kificho.
- Jamhuri yaiomba Mahakama muda kujibu hoja za Lissu kwa sababu walizoeleza kuwa hoja hizo zinahitaji majibu ya kisheria na utafiti.
Dar es Salaam. Kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu, imeahirishwa hadi Msajili wa Mahakama atakapopanga ratiba huku Lissu akiwasilisha hoja zake kupinga ushahidi wa kificho.
Akizungumza baada ya kusikilizwa kwa kesi leo Novemba 12, 2025, Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Dk. Rugemeleza Nshala, amesema kesi hiyo imeahirishwa baada ya Lissu kuwasilisha hoja ya kupinga matumizi ya chumba kilichotumika kwa shahidi P11, ambaye ni shahidi aliyepewa ulinzi na mahakama kwa kuficha utambulisho wake (shahidi wa kificho).
Mbele ya majaji watatu wakiongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru, Lissu amedai kuwa chumba kilichotumiwa hakimwezeshi shahidi kuonekana na jaji au hakimu wakati wa kutoa ushahidi, akifafanua kuwa mashahidi waliolindwa na Mahakama wanatakiwa kutoa ushahidi katika kizimba ambacho kinaruhusu jaji kumuona shahidi.
Pamoja na hayo ameeleza kuwa endapo Jamhuri ingehitaji kutumia kizimba maalum, ingelazimika kuiomba mahakama, jambo ambalo halikufanyika.

Lissu pia ameieleza Mahakama kwamba sheria inayotumika kuwalinda mashahidi haikutolewa kwa mujibu wa vigezo vya kisheria kwa kuwa haikuchapishwa kwenye Gazeti la Serikali, na kwamba tafiti zilizofanywa kwenye Maktaba ya Taifa, Bungeni na ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali hazikuonyesha sehemu ambapo sheria hiyo ilichapishwa.
Aidha, Lissu ameeleza sababu nyigine kuwa amri iliyowahi kutolewa na Jaji Mtembwa kuwa Jaji anayeendesha kesi inayowahusu mashahidi wa siri anatakiwa kupewa majina ya mashahidi hao na kuwafahamu huku akidai kuwa katika kesi yake majaji hawajapewa taarifa hizo na badala yake mashahidi wanajulikana na Jamhuri pekee.
Baada ya mashitaka hayo, upande wa Jamhuri unaoongozwa na Wakili wa Serikali Mkuu, Nassoro Katuga, uliomba Mahakama muda wa kutosha kujibu hoja za Lissu kwa sababu walizoeleza kuwa hoja hizo zinahitaji majibu ya kisheria na utafiti.
Lissu anatimiza siku 217 lumande tangu alipokamatwa na Jeshi la Polisi Aprili 9, 2025 alipokuwa katika mkutano wa kisiasa wa chama chake mkoani Ruvuma.
Kwa mara ya kwanza Lissu alifikishwa mahakamani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam Aprili 10, 2025 ambapo kwa sasa shauri lake linasikilizwa Mahakama Kuu.