Ifahamu startup ya Tanzania iliyotikisa anga la kimataifa
- Ni NovFeed iliyoshinda tuzo ya kimataifa ya kilimo teknolojia.
- Imepata zawadi ya Sh2.4 bilioni kutoka Taasisi ya Milken-Motsepe ya Marekani.
- Kampuni hii imebuni teknolojia ya kibayoteki inayoboresha malisho ya wanyama na pembejeo za kilimo.
Dar es Salaam. Matumaini ya kampuni zinazochipukia Tanzania kufanya vyema na kutambulika kwenye soko la kimataifa yanaendelea kudhihirika baada ya kampuni ya NovFeed kushinda tuzo ya kimataifa ya masuala ya kilimo teknolojia.
NovFeed, ni kampuni chipukizi iliyoanzishwa mwaka 2020 hapa nchini, imetunukiwa zawadi kubwa ya Dola za Marekani milioni 1 sawa na Sh2.4 bilioni kwa kushika nafasi ya kwanza katika tuzo za ‘Milken-Motsepe Prize in AgriTech’ zilizofanyika nchini Marekani hivi karibuni.
Kampuni hii imebuni teknolojia ya kibayoteki inayochakata taka kikaboni kuwa viambato mbadala vya protini.
Kwa kutumia vijiumbe asilia na kibayoteki vya viwandani ambavyo hugeuza taka hai kuwa bidhaa ya protini iliyokolea sana ikilenga kutengeneza pembejeo zenye lishe, zinazoweza kutumika kwenye mfumo wa chakula, hivyo kuwezesha sekta za nyama na ufugaji wa samaki kupata bidhaa za chakula.
Tuzo hizo zilizinduliwa Aprili 2021, ambapo zaidi ya watu 3,300 kutoka nchi 105 katika mabara sita walijiandikisha kuwania tuzo ya Milken-Motsepe kwenye kipengele cha teknolojia ya kilimo (AgriTech).
Teknolojia hii muhimu imeipata NovFeed tuzo ya kwanza kabisa ya Milken-Motsepe kwenye kipengele cha AgriTech, ikitolewa na Taasisi ya Milken-Motsepe.
Zawadi hiyo imetolewa kutambua na kutuza suluhu bunifu zinatatua changamoto kubwa zinazoikumba sekta ya kilimo duniani.
Teknolojia ya NovFeed inaboresha mfumo wa upatikanaji wa chakula, ikitoa njia rafiki kwa mazingira kwa kutoa viambato vya protini vyenye ubora wa juu na mbolea ya mimea huku ikipunguza upotevu wa rutuba.
Soma zaidi:
- Mambo muhimu yatakayozisaidia kampuni zinazochipukia Tanzania kukua
- Startups za Tanzania zilizotamba mwaka 2018
- Starups nne Zanzibar zapenya shindano la Seedstars
Kwa kutumia taka za kikaboni kama malighafi, NovFeed ina uwezo wa kutoa chanzo endelevu cha protini ambacho kinaweza kutumika katika bidhaa mbalimbali za chakula, pamoja na malisho ya wanyama na njia mbadala za mimea.
Mbolea ya mimea inayozalishwa na NovFeed pia ni mafanikio katika kilimo endelevu, ikitoa chanzo cha asili na kilichokolea sawia kwa virutubisho vya mazao.
Hii sio tu inapunguza haja ya mbolea za kemikali lakini pia inaboresha afya ya udongo na kupunguza uzalishaji wa gesi chafu.
“Washindi ni mfano wa ukweli kwamba mawazo ya ujasiri, yanayoishi, na mabadiliko yanaweza kutoka popote,” alisema Dk Emily Church, Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Milken Institute for Strategic Philanthropy Mei Mosi mwaka huu wakati wa utoaji wa tuzo.
“Kuleta vipaji mbele na kusaidia wajasiriamali ni lengo la makusudi la ushindani. Haiishii hapo. Mtandao uliopanuliwa wa wawekezaji na wadau waliojengwa katika mpango huu unazipa timu zinazoshinda fursa za kuendelea kuvumbua na kustawi,” alisisitiza Church.
Ushindi wa tuzo hii ya teknolojia kwa kampuni chipukizi ya Kitanzania ni mfano mzuri kwa wavumbuzi nchini, kutumia ujasiriamali na teknolojia kuleta mabadiliko chanya duniani.
Pia ushindi wa NovFeed sio tu ushindi kwa kampuni lakini kwa tasnia nzima ya kilimo.
Ulimwengu unapokabiliwa na changamoto zinazoongezeka za chakula na mazingira, suluhu ya kibunifu zitakuwa muhimu katika kujenga mfumo wa chakula endelevu na sawa kwa wote.
Latest