Hizi ndizo kampuni mbili zilizopoteza soko la hisa Dar Oktoba 29
- Benki hiyo imeongoza kwa kuuza kiwango kikubwa cha hisa katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) kwa asilimia 98.8.
- Hata hivyo, thamani ya hisa zake imeshuka kwa asilimia tano na kuwafanya wawekezaji wake kupoteza Sh5 kwa kila hisa moja.
- Thamani ya hisa za benki ya KCB na Shirika la ndege la Kenya Airways (KA) zimepanda kwa viwango tofauti.
Dar es Salaam. Licha ya benki ya CRDB kuongoza kwa kuuza kiwango kikubwa cha hisa katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) leo, thamani ya hisa zake imeshuka kwa asilimia tano na kuwafanya wawekezaji wake kupoteza Sh5 kwa kila hisa moja.
Ripoti ya siku iliyotolewa leo (Oktoba 29, 2019) na DSE inaeleza kuwa CRDB imeuza hisa 938,310 sawa na asilimia 98.8 ya hisa zote zilizouzwa sokoni leo ikifuatiwa kwa mbali na kampuni ya uwekezaji ya NICO ambayo imeuza hisa 9,250 na kampuni ya saruji ya Twiga (TPCC) iliyouza hisa 1,556.
Hata hivyo, usiku wa leo unaweza isiwe mzuri kwa wawekezaji wa benki hiyo kwa sababu hadi soko linafungwa jioni, thamani ya hisa moja ya CRDB ilikuwa Sh95 kutoka Sh100 iliyorekodiwa jana.
CRDB imeungana na kampuni ya bia ya Afrika Mashariki (EABL) ambayo thamani ya hisa zake imeshuka kwa asilimia 0.47 ambapo thamani ya hisa moja ilikuwa Sh4,280 kutoka Sh4,300 iliyorekodiwa jana.
Zinazohusiana:
- M-pesa, intaneti vyachangia Vodacom Tanzania kupata faida ya Sh90 bilioni
- Wawekezaji wa Acacia soko la hisa Dar tabasamu tupu
- Maumivu kwa wawekezaji wa kampuni ya bia soko la hisa Dar
Wakati thamani ya hisa za CRDB na EABL zikishuka, benki ya KCB na Shirika la ndege la Kenya Airways (KA) zina kila sababu ya kutabasamu kwa sababu thamani ya hisa zao zimepanda kwa viwango tofauti.
Thamani ya hisa za KCB zimepanda kwa asilimia 2.06 ambapo mpaka soko linafungwa thamani ya hisa moja ilikuwa Sh990 kutoka Sh970 iliyorekodiwa jana ambapo wawekezaji wake wameweka kibindoni Sh20 kwa kila hisa moja.
KA nayo thamani ya hisa zake imepanda kwa asilimia 8.33, kampuni JHL (asilimia 1.29) na kampuni ya habari ya NMG (asilimia 1.09).
Kampuni zilizobaki viwango vyake vibaki kama vilivyokuwepo jana zikiwemo Vodacom, benki ya DCB na Acacia.