HESLB kuwabana wanasheria zaidi ya 5,000 mikopo elimu ya juu
Mkuu wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa vitendo Tanzania (LST) Jaji Dk Benhajj Masoud (katikati) na Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), Abdul-Razaq Bardu (kushoto) wakionesha hati ya makubaliano yatakayoiwezesha HESLB kudai zaidi ya Sh10.6 bilioni kutoka kwa wanufaika 5,065 waliokua wanafunzi wa taasisi hiyo kati ya mwaka 2008 na 2015. Hafla hiyo ilifanyika Juni 21, 2022 Jijini Dar es Salaam. Picha| HESLB.
- Ni waliokuwa wanafunzi wa “Law School of Tanzania” kati ya 2008 na 2015.
- Wanatakiwa kurudisha zaidi ya Sh10.6 bilioni.
- Bodi ya mikopo kuanza kuwatafuta Julai 1, 2022.
Dar es Salaam. Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imesema wanasheria 5,065 waliokopeshwa zaidi ya Sh10.6 bilioni wakiwa wanafunzi wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria Kwa Vitendo Tanzania (Law School of Tanzania (LST)) wanatakiwa kurejesha mikopo hiyo ili iwanufaishe wanafunzi wengine wa elimu ya juu.
Wanasheria hao ni wale walionufaika na mikopo ya elimu wakiwa wanafunzi wa LST kati ya mwaka 2008 na 2015 wakisoma Stashahada ya Juu ya Uanasheria kwa Vitendo (Post Graduate Diploma in Legal Practice) wakati sheria ya HESLB ilipokua hairuhusu wanafunzi wa LST kukopeshwa.
Sheria ya bodi hiyo ilirekebishwa mwaka 2014 na kuruhusu wanafunzi wa LST kukopeshwa mikopo kwa ajili ya kugharamia ada na mahitaji mengine wakiwa masomoni.
Kwa mujibu wa makubaliano yaliyosainiwa jijini Dar es salaam Juni 21, 2022 na watendaji wakuu wa taasisi hizo, wanasheria hao ni wale waliosoma kupitia kundi (cohort) la kwanza hadi 19 na kukopeshwa na Serikali kupitia LST.
“Tunashukuru kuwa mikataba waliyosaini walipokua wanafunzi-wanasheria ipo wazi kuwa LST inaweza kuipa kazi ya kukusanya madeni haya taasisi yoyote ya umma au binafsi.
Soma zaidi:
- Waombaji 10,452 Heslb wapewa siku nne kurekebisha kasoro
- Heslb yaanika kozi zitakazopewa kipaumbele mikopo elimu ya juu 2019-2020
- TCU yaanika sifa za wanafunzi kujiunga vyuo vikuu Tanzania
Hivyo baada ya mazungumzo tangu 2019, leo tumefikia hatua hii,” amesema Jaji Dk Benhajj Masoud, Mkuu wa LST katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo.
Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Abdul-Razaq Badru amesema HESLB ina uzoefu na utayari wa kutekeleza jukumu hilo na kuwakumbusha wanufaika hao kujitokeza na kurejesha.
“Tumejipanga kuanza kuwahudumia kuanzia Julai 1, 2022 … hivyo tunatoa wito kwa wateja wetu hawa kurejesha fedha hizi pamoja na zile walizokopeshwa wakiwa wanafunzi wa shahada za kwanza ili ziwanufaishe vijana wengine wa kitanzania wanaohitaji,” amesema Badru.