Hapana: Siyo lazima kupima Uviko-19 kabla ya kupata chanjo
- Kila mtu ana haki ya kupata chanjo.
- Sio lazima mtu anayetaka kupata chanjo apime Corona.
Dar es Salaam. Wakati dunia ikiendelea na mapambano juu ya ugonjwa wa Uviko-19 na kuhamasisha chanjo, kumeibuka taarifa za uzushi kuwa ili uweze kupata chanjo ya ugonjwa huo ni lazima upime na uwe tayari umeshaambukizwa ugonjwa huo.
Taarifa hizo zinazosambaa kwenye jamii na mitandao ya kijamii sio za kweli.
Shirika la Afya Duniani (WHO) inasema kila mtu ana haki ya kupata chanjo, kwa wakati wowote ili kuzuia kusambaa zaidi kwa ugonjwa huo na hatari za vifo.
“Siyo lazima mtu anayetaka kupata chanjo awe amewahi kupata ugonjwa huo au apime kwanza ndipo apewe chanjo,” anasema Dk Phionah Atuhebwe, Afisa Chanjo kutoka WHO.
Hata hivyo, Afisa huyo amesema ikiwa vipimo vitaonyesha umeambukizwa Uviko-19 unatakiwa kujitenga na kupata matibabu kabla ya kupata chanjo ya ugonjwa huo.
Zinazohusiana
-
Tatizo la afya ya akili sasa kutupiwa macho
-
Unachoweza kufanya kujikinga na maambukizi mapya ya corona
Nani haruhusiwi kupata chanjo?
Sambamba na hayo WHO imeainisha mazingira ambayo mtu hataruhusiwa kupata chanjo.
Hutaruhusiwa kupata chanjo ikiwa una mzio na moja ya viambata vilivyopo kwenye chanjo za Uviko-19 ili kuzuia madhara zaidi ya kiafya yanayoweza kutokea.
Ikiwa joto lako la mwili limezidi nyuzijoto 38 hairisha mpango wa kupata chanjo mpaka joto litakaposhuka.
Hutaruhusiwa kupata chanjo ikiwa umethibitisha kupata Uviko 19 siku za karibuni. Wataalamu wanashauri mgonjwa asubiri hadi muda wa kujitenga ukamilike na dalili za ugonjwa huo ziwe zimeisha.
Kwa wanaotumia dawa za kupunguza damu wanashauriwa kumtaarifu mtoa chanjo kabla ya kupata chanjo yoyote ya Uviko-19.
WHO inasema Japo ni salama kupata chanjo ukiwa kwenye hali hiyo lakini kutoa taarifa mapema ni muhimu kwani kutamsaidia mtoa huduma kukupa ushauri na kutoa huduma za ziada zitakapohitajika.
Latest
