Guteress: Shughuli za kibinadamu zinahatarisha uwepo wa ‘spishi za kipekee’
- Atoa wito wa kila mmoja kufanya tathimini ya wajibu wake kulinda misitu minene, bahari, maziwa pamoja na mito.
- Asisitiza utekelezaji wa mkataba wa CITES.
- UNEP washauri kuimarisha uhusiano na jamii za asili kutasaidia kuongeza utunzaji wa spishi hizo.
Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) Antonio Guterres amesema shughuli za binadamu zimekuwa sababu kubwa inayohatarisha uwepo wa spishi za kipekee ulimwenguni huku akitoa wito kwa kila mmoja kutathmini wajibu wake katika ulinzi wa spishi hizo.
Guteress aliyekuwa akitoa ujumbe katika siku ya kimataifa ya wanyamapori ambayo huadhimishwa Machi 3 kila mwaka amesema kutotimizwa kwa wajibu huo kumesababisha kutoweka kwa misitu minene, bahari, maziwa pamoja na mito.
Kutokana na shughuli za binadamu, zaidi ya spishi milioni za uoto ziko hatarini kutoweka kutokana na uharibifu wa makazi yao, uchafuzi kutokana na mafuta kisukuku pamoja na janga la tabianchi linalokua kwa kasi kila uchao.
Kwa mujibu wa Guteress, ni wakati sahihi wa kutekeleza Mkataba wa Kimataifa wa Biashara ya Viumbe Vilivyo Hatarini Kutoweka (CITES) kama nyenzo ya ulinzi kwa spishi hizo zinazoendelea kupotea.
“Mwaka huu ni mwaka wa 50 tangu upitishwe na umesaidia sana kulinda maelfu ya mimea na wanyama. Na mkataba wa mwaka jana wa Kunming-Montreal kuhusu mfumo wa bayonuai duniani uliashiria hatua muhimu kuelekea njia ya kuponya sayari yetu,” amesema Guteress.
Zinazohusiana
-
Sekta ya utalii: Nguzo muhimu kupambana na Uviko-19
-
Zifahamu mbuga za wanyama kubwa zaidi Afrika Mashariki
Inger Andersen, ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira Duniani (UNEP), amesema pamoja na mikataba iliyoPo, kuimarisha ubia na watu wa jamii ya asili na jamii kwenye maeneo husika ni miongoni mwa nyenzo ya ulinzi itakayosaidia.
“tukubali kuwa watu wa jamii ya asili wanafahamu zaidi uhifadhi kuliko hata wanasayansi, katika siku ya wanyamapori duniani tuahidi kuimarisha ubia na mazigira, kwa sababu mustakabali wetu na wa spishi zote duniani unategemea ubia huo,” amehitimisha Andersen.
Historia ya siku hii
Disemba 20 mwaka 2013, mkutano wa 68 wa Baraza Kuu la UN uliamua kutangaza Machi 3 kila mwaka kuwa siku ya wanyamapori duniani kusherehekea na kuinua uelewa wa wanyama na mimea duniani.
Tarehe hiyo ndiyo siku ambayo mwezi Machi mwaka 1973 ulipitishwa mkataba wa kimataifa wa biashara ya wanyama na mimea iliyo hatarini kutoweka wa CITES.