Falme za kiarabu yasitisha safari za ndege kutoka Kenya, Tanzania
- Imesitisha ndege za abiria kutoka Tanzania Kenya, Ethiopia, na Nigeria.
- Ni hatua za kujikinga na Uviko-19.
- Ghana na Uganda nazo zawekewa masharti magumu.
Dar es Salaam. Kama umepanga safari ya kwenda Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) mwisho wa wiki hii kwa ajili ya mapumziko na shughuli za kibiashara, basi una bahati mbaya.
Nchi hiyo ya mashariki ya kati itasitisha safari za ndege za abiria kutoka Tanzania Kenya, Ethiopia, na Nigeria itakapofika Jumamosi Desemba 25, 2021 huku ikiongeza vikwazo vya usafiri kwa ndege za Uganda na Ghana.
Uamuzi huo pia unawazuia wasafiri wa kimataifa waliokuwa katika nchi hizo nne siku 14 kabla ya kuwasili UAE.
“Operesheni za ndege zitaendelea kusafirisha abiria kutoka UAE hadi nchi hizo,” imeeleza taarifa ya Mamlaka ya Kitaifa ya Kudhibiti Dharura na Majanga (NCEMA) na Mamlaka ya Usafiri wa Anga (GCAA) za nchi hiyo.
Hatua hizo mpya zitaanza kutekelezwa kuanzia saa moja na nusu usiku wa Jumamosi.
Zuio hilo la safari za ndege halitawahusu raia wa UAE, wanadiplomasia na wamiliki wa makazi ya dhahabu, ingawa wanatakiwa kuwasilisha majibu ya vipimo vya Uviko-19 ndani ya saa 48 baada ya kuanza safari.
Vile vile wanatakiwa kufanyiwa kipimo cha haraka (Rapid-PCR) kwenye uwanja wa ndege saa sita kabla ya kuondoka katika nchi zao na katika viwanja vya ndege vya UAE.
Pia watatakiwa kukaa karantini kwa siku 10 na kupima kipimo cha Uviko-19 kwa njia ya pua katika siku ya tisa ya kukaa kwao UAE.
Soma zaidi:
- Waziri azungumzia ndege za ATCL kuchelewa, kuahirisha safari
- Shirika la ndege la Ethiopia limesitisha safari zote za ndege aina ya Boeing 737
- ATCL inavyojitanua kimataifa
GCAA) imesema kuwa wale wanaowasili kutoka nchi hizo nne kupitia mataifa mengine lazima wakae katika nchi za mwisho kwa angalau siku 14 kabla ya kuruhusiwa kuingia UAE.
“Raia wa UAE wamezuiwa kusafiri kwenda nchi nne za Afrika isipokuwa kwa kesi za matibabu ya dharura nchini humo, wajumbe rasmi, na ufadhili wa masomo,” imeeleza taarifa ya mamlaka hizo mbili.
Kwa abiria wanaotoka Uganda na Ghana, nchi hiyo imeweka masharti mapya ya usafiri kwa wasafiri wanaowasili kwa ndege za moja kwa moja ikiwemo wawasilishe kipimo cha Uviko-19 ndani ya saa 48 na wakapime kipimo cha haraka katika uwanja wa ndege ndani ya saa sita baada ya kuondoka.
Wale wanaosafiri kwenda UAE lazima waonyeshe kipimo cha Uviko-19 kilichopatikana ndani ya saa 48 na majibu ya kipimo cha haraka kwenye uwanja wa ndege wa eneo lao kuu la kuondoka ndani ya saa sita za kusafiri.
Pia watapima kipimo cha haraka katika uwanja wa ndege wa mpito kabla ya kuruhusiwa kuingia UAE.
Hatua hizo ni kuimarisha mapambano dhidi ya kirusi kipya cha Uviko-19 aina ya Omicron ambacho kinasambaa kwa kasi duniani.