Diamond, Nandy kuiwakilisha Tanzania tamasha la Afrika Mei 25
- Wasanii hao wataungana na wenzao wa nchi za Afrika kushehereka siku ya bara hilo.
- Tamasha hilo litafanyika mtandaoni kuonyesha umoja wa Afrika dhidi ya janga la Corona.
- Unaweza kufuatilia mubashara kwenye mtandao wa Youtube au kwenye chaneli ya MTV.
Dar es Salaam. Ni nini maana ya Afrika kama siyo watu wake? Ndiyo! ngoma za kitamaduni, mavazi na sauti zenye mitetemo ya Kiafrika ndiyo Afrika yenyewe.
Tumeshuhudia matamasha mengi ya mtandaoni lakini ni kweli halikuwepo lile linalokonga Uafrika. Na sasa, limepata nafasi.
Tamasha hilo ambalo linatarajiwa kufanywa kwa njia ya mtandao Siku ya Afrika(Africa Day) Mei 25, 2020 linalenga kuliweka bara hilo katika nafasi moja ya ushirikiano hasa kipindi hiki cha mlipuko wa janga la Corona.
Shoo hiyo (#IAmWAN) itakayodumu kwa saa mbili itawakutanisha nguli wa muziki wa Afrika ambao kutoka katika nchi zao watakutana pamoja mtandaoni kukonga nyoyo za mashabiki wao ambao hawajaonana nao kwa muda sasa.
Tanzania itawakilishwa na wasanii wawili; Diamond Platnumz na Nandy huku Kenya itawatoa Sauti Sol na Bebe Cool itaiwakilisha Uganda.
Lakini atakuwepo mama “Pata pata” mwenye Grammy (tuzo za kimataifa zinazotambua mchango wa watu kwenye sekta ya muziki) yake siyo mwingine ni Angélique Kidjo wa nchi ya Benin.
Zinazohusiana
- Tamasha la ‘Urithi Festival’ kufanyika mikoani kila mwaka
- Tamasha kuwaunga mkono wapambanaji wa Corona kufanyika Aprili 18
- Hawa ndiyo wanamuziki wa kike wanaotikisa dunia kwa wafuasi wengi Youtube
Tulia! Bado orodha inaendelea. Kutoka Afrika Magharibi, yupo Burna Boy, Yemi Alade, Teni, Tiwa Savage, Seun Kuti, Rema na Adekunle Gold hao wote ni kutoka Nigeria.
Kule kwa Madiba, watakaotoa burudani ni rapa AKA na mwana dada aliyesumbua spika za watu kwa kibao cha “John Cena”, Sho Madjozi.
Hakika haiwezi kukamilika bila miuno ya Kikongo kutoka kwa Fally Ipupa au vipi? Na kama haujafahamu bado, atakayesherehesha shoo hii ni muigizaji maarufu mwenye cheo chake. Ni Idriss Elba.
Kufurahia shoo hiyo, siyo haba ukawa na bando la kutosha kutazama mtandao wa YouTube au chaneli ya MTV kwenye king’amuzi. Fuatilia kurasa za WanAfrica kufahamu orodha yote ya wasanii ambao utawatazama.
Tamsha hilo litazidi kudhihirisha umoja walionao Wafrika katika maendeleo ya bara lao.
Latest