Corona: Mashirika yasiyo ya kiserikali yanavyopambana na habari za uzushi Tanzania
- Ni kwa kutoa elimu na habari zilizo sahihi kwa wananchi wanaowahudumia.
- Yataka vyombo vya kuzingatia weledi na taalum katika utoaji habari.
Mwanza. Wakati dunia ikiendelea kutoa chanjo dhidi ya ugonjwa wa Corona, baadhi ya mashirika yasiyo ya kiserikali nchini Tanzania yamesema habari za uzushi zimekuwa zikiwapata wakati mgumu katika elimu kwenye jamii kuhusu ugonjwa huo.
Corona siyo tu imeathiri afya za watu, bali imeibua janga nyingine la habari za uzushi ambazo zinatengenezwa na watu wenye nia mbaya ili kunufaika na ugonjwa huo ikiwemo kujipatia fedha isivyo halali.
Mratibu wa shirika lisilo la kiserikali la Rarways la jijini Mwanza, Mary Mushi anasema kimsingi taarifa zozote za upotoshaji zinasababisha taharuki kwa wananchi na wakati mwingine huleta uoga katika kujikinga na Corona.
“Ni kweli wakati mwingine tunakutana na taarifa zisizo sahihi na zinatupa wakati mgumu hadi tunakutana na taasisi husika kutupa ukweli wa jambo hilo,” amesema Mushi wakati akiongea na Nukta Habari (www.nukta.co.tz).
Mushi amesema wanatoa elimu juu ya kujikinga na Corona lakini uwepo wa habari nyingi za uzushi kuhusu ugonjwa huo zinakwamisha juhudi za kuwakwamua wananchi kwenye janga hilo.
Hata hivyo, anasema mashirika yamekuwa makini kwa kufuata misingi na taratibu za Serikali katika kutoa taarifa za Corona na pale panapotokea mkanganyiko huwasiliana na wataalam wa afya ili kuwalinda watu wanaowahudumia.
“Uelewa kwenye jamii kuhusiana na jambo hilo (Corona) bado ni mdogo ingawa kama viongozi kwenye taasisi tunaofanya kazi karibu na watu tunajitahidi kuwapa taarifa na elimu sahihi ya namna ya kuchukua taarifa zinazotolewa na mamlaka husika,” amesema Mushi.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) hadi jana Juni 18, 2021, kulikuwa na wagonjwa 177.2 wa COVID-19 na vifo milioni 3.8 kote duniani.
Ili kukabiliana na habari hizo, vyombo vya habari hasa vya mtandaoni vimetakiwa kuwa mstari wa mbele kutoa taarifa sahihi kuhusu ugonjwa wa Corona ili kupunguza madhara kwenye jamii ya kutumia taarifa zisizo sahihi.
Mratibu wa Sheria, Utetezi na Uzingatiaji wa shirika lisilo la kiserikali la WoteSawa, Joseph Mkoji amevitaka vyombo vya habari kufanya kazi kwa weledi wa taalauma hususani kwenye masuala yanayohusu mambo ya kisayansi.
“Kimsingi kutoa taarifa zisizo sahihi zinazohusina na ugonjwa wa COVID-19 ni kinyume cha sheria, ni vyema kuzingatia taarifa zinazotolewa na mamlaka ya afya ili kutoingia mgogoro na Serikali,” amesema Mkoji.
Miongoni mwa vyombo vya habari ambavyo viko mstari wa mbele kutoa elimu ya kujikinga na COVID-19 ni Nukta Habari (www.nukta.co.tz) ambapo unaweza kufuatilia zaidi habari zake kupitia ukurasa wake wa Facebook wa @NukataFakti.