CAG aibua utata mabilioni ya fedha za ‘Plea Bargaining’
- Badhi ya fedha zilitunzwa kwenye akaunti binafsi za watu.
- Kati ya Sh6.1 bilioni zilizokusanywa ni Sh1.3 bilioni zilipelekwa hazina.
Dar es Salaam. Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere amebaini mapungufu ya fedha zilizokusanywa za adhabu ya makubaliano baada ya kukiri kosa (Plea bargaining) ikiwemo kutunza katika akaunti za benki za watu binafsi.
“Nilifanya ukaguzi maalumu kuhusu uendeshaji wa usimamizi wa mikataba ya maridhiano na kukiri makosa (plea bargaining) nilibaini fedha zilizotaifishwa na kuwekwa kimakosa kwenye akaunti ya makubaliano ya hiari ni Sh6.1 bilioni na pesa zilizokabidhiwa hazina ni Sh1.3 bilioni,” amesema CAG.
Hii si mara ya kwanza kwa Serikali kukiri juu ya upotevu wa fedha hizo ambazo ukusanywaji wake ulishika kasi katika Serikali ya awamu ya tano iliyokuwa ikiongozwa na Hayati Rais John Magufuli.
Machi 31 mwaka huu, Rais Samia Suluhu Hassan alikiri upotevu wa fedha za ‘Plea Bargaining’ wakati wa kuzindua tume itakayoangalia namna ya kuboresha mfumo wa haki jinai kwenye viwanja vya Ikulu Dodoma.
Rai Samia aliagiza uchunguzi wa kina kufanyika juu ya fedha hizo zilizokusanywa.
Pia CAG Kichere amebaini makosa mengine ya mfumo huo ikiwemo mali zilizotaifishwa kutokuorodheshwa kwenye daftari maaalum pamoja na malalamiko ya uonevu kutoka kwa waathirika wa mfumo wa ukusanyaji wa pesa hizo.
Soma zaidi
Iundwe tume huru kuchunguza mfumo wa ‘plea bargaining’
Akiwasilisha ripoti yake ya mwaka 2021/22, CAG Kichere amependekeza kundwa kwa tume huru itakayochunguza mfumo mzima wa ukusanyaji wa fedha za ‘plea bargaining’.
“Napendekeza iundwe tume huru ya kuchunguza uwezekano wa ukiukwaji wa maadili na matumizi mabaya ya ofisi ya umma katika mchakato wa kukiri kosa na kutaifisha mali za watuhumiwa ‘Plea bargain’,” amesema Kichere.
Mkaguzi huyo wa hesabu za Serikali amesema kuwa licha ya uwepo wa vyombo vya ulinzi na usalama vinavyoshughulikia jambo hilo ipo haja kubwa ya uundwaji wa tume hiyo.
Latest