Rais Samia apokea ripoti CAG, TAKUKURU na PPRA aagiza utekelezaji wa haraka
- Serikali itachukua hatua kwa mujibu wa sheria kulingana na mapendekezo yaliyotolewa ili kuondoa mapungufu yaliyobainishwa.
- CAG Kichere amebainisha kuwa kwa miaka mingi baadhi ya mapendekezo hayo hayafanyiwi kazi ipasavyo, hali inayochangia hasara na kudhoofisha uwajibikaji
Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amepokea ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) zilizotoa tathmini ya utekelezaji wa majukumu ya taasisi zao kwa mwaka wa fedha 2024/2025.
Rais Samia amepokea ripoti hizo leo Machi 30, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam ikiwa ni hatua inayotimiza takwa la kisheria la taasisi hizo kuwasilisha taarifa zake kabla ya kumalizika kwa robo ya kwanza ya mwaka.
Akizungumza mara baada ya kupokea ripoti hizo, Rais Samia amesema Serikali itachukua hatua kwa mujibu wa sheria kulingana na mapendekezo yaliyotolewa ili kuondoa mapungufu yaliyobainishwa kwa lengo la kuimarisha usimamizi na uwajibikaji wa rasilimali za umma.
“Na hapa nimuelekeze Katibu Mkuu kiongozi kusimamia kwa karibu tathmini ya utekelezaji wa mapendekezo yote yaliyotolewa na taasisi hizi,” ameagiza Rais Samia.
CAG, TAKUKURU, PPRA waanika madudu
CAG Charles Kichere, amesema katika mwaka wa fedha 2024/2025 ofisi yake imefanya jumla ya kaguzi 1,553 za aina mbalimbali.
Kati ya kaguzi hiyo CAG amebaini masuala, madudu na hasara zilizotengenezwa na taasisi za umma 22 ikiwemo Sh119.1 bilioni ya ATCL iliyotengenezwa katika mwaka wa fedha 2024/25 pamoja na jumla ya hasara ya Sh748 bilioni iliyorekodiwa tangu kuanzishwa kwakwe.
Mbali na ATCL Kichere amebaini jumla ya Sh7.25 bilioni ambazo hazikukusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa zaidi ya miaka 17 na Bohari ya Dawa (MSD) kupokea dawa na vifaa tiba vyenye thamani ya Sh20.28 bilioni vilivyokuwa na muda mfupi wa matumizi, kinyume na miongozo iliyopo.
Kwa upande wa PPRA, Mkurugenzi Mkuu Dennis Simba amebaisha kuwa taasisi nunuzi 756 kati ya 943 hazikutenga asilimia 30 ya bajeti zao kwa makundi maalum, kinyume na matakwa ya sheria. Pia taasisi 22 zilibainika kutoa zabuni kwa upendeleo usiostahili, hatua iliyosababisha ongezeko la gharama kwa zaidi ya Sh5.1 bilioni.
Aidha, Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Crispin Chalamila, amesema shirika hilo limeokoa Sh14.5 bilioni kuanzia Julai 2024 hadi Juni 2025 kupitia operesheni za uchunguzi.
Kati ya fedha hizo, Sh10.1bilioni ni fedha taslimu na Sh 4.4 bilioni ilidhibitiwa sambamba na kurejesha vifaa na mali zilizoelekezwa kwenye utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Hata hivyo, CAG Kichere amebainisha kuwa kwa miaka mingi baadhi ya mapendekezo hayo hayafanyiwi kazi ipasavyo, hali inayochangia hasara kwa Serikali na kudhoofisha uwajibikaji katika taasisi za umma.
Kwa sasa ripoti zilizotolewa zinatarajiwa kujadiliwa bungeni katika mkutano wa Bunge unaoanza kesho, Machi 31, 2026, ambapo wabunge watajadili hoja na mapendekezo yaliyobainishwa.
Latest