Bunge lapitisha Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya NHC
- Ni pamoja na kifungu cha 23 kinapendekezwa kurekebishwa ili kuongeza ruzuku kama chanzo cha mapato ya Shirika.
Dar es Salaam. Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) linatarajiwa kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yake, baada ya Bunge la Tanzania kupitisha Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya NHC wa mwaka 2025 ikiwemo kuipa Bodi ya Wakurugenzi uwezo wa kuwekeza bila kuhitaji idhini ya Waziri wa Ardhi.
Marekebisho hayo yanaifanya NHC kuwa na uhuru zaidi katika uwekezaji na utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa masharti ya Sheria ya Mamlaka na Majukumu ya Msajili wa Hazina, Sura ya 370 kuhusu uwekezaji wa mashirika ya umma
Muswada huo, ambao umegawanyika katika sehemu mbili kuu, umependekeza mabadiliko katika vifungu mbalimbali vya Sheria ya Shirika la Nyumba la Taifa, Sura ya 295.
Miongoni mwa vipengele vilivyoboreshwa ni kifungu cha 5 kinacholenga kuongeza na kuboresha majukumu ya bodi ya shirika, pamoja na kuongeza kifungu kipya cha 5A kitakachoruhusu uundwaji wa kamati maalum za kusaidia utekelezaji wa majukumu ya bodi.
Kifungu cha 9 kimepanuliwa ili mkurugenzi mkuu aweze kukasimu mamlaka ya kusaini nyaraka mbalimbali kwa maafisa waandamizi badala ya mikataba ya upangishaji pekee.
Hii inalenga kurahisisha utekelezaji wa shughuli za Shirika kwa wakati.
Aidha, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Deogratius Ndejembi aliyekuwa akizungumza bungeni jijini Dodoma amewaambia wabunge kuwa Vifungu vya 12 na 13 kwenye muswada huo vimeondoa utaratibu wa waajiri kukata kodi ya nyumba kutoka kwenye mishahara ya wafanyakazi wapangaji.
“Lengo la marekebisho haya ni kuongeza uwajibikaji wa moja kwa moja kwa mpangaji katika kulipa kodi ili kurahisisha ukusanyaji wa kodi za nyumba za shirika,” amebainisha Waziri
Hata hivyo, Ndejembi amesisitiza kuwa marekebisho ya vifungu vya 15 hadi 17 yanalenga kuongeza adhabu kwa makosa kama vile kutoa taarifa za uongo, kuficha siri za shirika, au kuzuia ukaguzi.
“Lengo la marekebisho haya ni kuwezesha adhabu kutolewa kulingana na hali halisi ya thamani ya fedha na uzito wa makosa pamoja na athari za makosa hayo ,” amesisitiza Waziri Ndejembi.
Kwa upande wa uongozi, kifungu cha 18 sasa kinampa Rais mamlaka ya kumteua mkurugenzi mkuu wa shirika, badala ya waziri.
Marekebisho mengine ni pamoja na kuongeza ruzuku kama chanzo cha mapato ya shirika na kuondoa masharti ya zamani kama mfuko wa dhamana na akiba, ambayo hayajawahi kutumika.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Timotheo Mnzava ameleza kuwa maboresho ya sheria kwa ajili ya utekelezaji bora wa shughuli za NHC yatakuwa na tija zaidi iwapo Shirika litawezeshwa kwa kusimamiwa katika ukusanyaji wa madeni na utekelezaji wa miradi yake.
“Kamati inashauri Serikali na taasisi zake ambazo ni wapangaji katika nyumba za Shirika zilipe madeni yote ili liweze kufanya kazi inavyostahili,” amefafanua Mnzava.
Latest



