BoT yatoa maagizo mazito taasisi za huduma ndogo za kifedha

July 1, 2025 6:21 pm · Goodluck Gustaph
Share
Tweet
Copy Link
  • Yazitaka kujiunga na vyama vya watoa huduma ndogo za kifedha vya TAMFI na TAMIU.
  • Watakaokaidi kunyang’anywa leseni. 

Dar es Salaam. Benki Kuu ya Tanzania (BOT) imetangaza hatua kali dhidi ya taasisi za huduma ndogo za kifedha ambazo hazitazingatia utaratibu wa kujiunga na vyama vya watoa huduma ndogo za kifedha ikiwemo Chama cha Taasisi za Fedha Ndogo Tanzania (TAMFI).

Chama kingine ambacho taasisi hizo zitakiwa kujunga ni Muungano wa Taasisi zinazotoa mikopo, Akiba na Huduma nyingine za Kifedha (TAMIU).

Kauli hiyo imetolewa na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Emmanuel Tutuba leo Julai 01, 2025 wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa utaratibu wa usimamizi binafsi kwa taasisi za huduma ndogo za fedha za daraja la pili, BoT na vyama vya watoa huduma ndogo za fedha iliyofanyika jijini Dar es salaam.

“Sisi kama kama Benki Kuu tutaendela kutoa taarifa kwa umma kuhusu kuanzishwa kwa utaratibu huu mpya wa usimamizi binafsi kwa taasisi za huduma ndogo za fedha  za daraja la pili, hivyo naomba kusisitiza kuwa taasisi zote za huduma ndogo za fedha daraja la pili zinatakiwa kujiunga ama kujisajili na taasisi au chama kimojawapo kati ya TAMFI au TAIMU ndani ya kipindi cha miezi sita,” amesema Tutuba.

Gavana Tutuba ametoa rai kwa taasisi na watoa huduma ndogo za kifedha daraja la pili kuhakikisha wanazingatia utaratibu huo wa kujisajili chini ya vyama hivyo viwili ili waendelee kutoa huduma.

“ Zoezi hili la kujisajili linatakiwa kutekelezwa kuanzia leo tarehe 1 Julai, 2025 hadi mwishoni wa Disemba 2025, kwa hivyo tutakuwa na kipindi cha miezi sita na baada ya hapo taasisi ambayo haijajisajili kufikia disemba tutainyang’anya leseni,” amesema Gavana Tutuba.

Sekta ya huduma ndogo za kifedha ina umuhimu mkubwa katika kukuza uchumi wa wananchi wa kipato cha chini, hivyo usimamizi madhubuti unahitajika kuhakikisha maendeleo endelevu.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW