Biashara, watu binafsi wanavyonufaika mikopo sekta binafsi Tanzania
- Sehemu kubwa ya mikopo kwa sekta binafsi imeelekezwa kwa watu binafsi au kaya ambazo zilipata wastani wa asilimia 29.6 ya mikopo yote na shughuli za biashara (asilimia 17.9).
- Mikopo kwa sekta binafsi imeongezeka kwa wastani wa asilimia 9.1 katika mwaka ulioishia Januari 2020 ikilinganishwa na asilimia 7.3 iliyorekidiwa katika kipindi kama hicho mwaka 2019.
Dar es Salaam. Wakati mikopo inayoelekezwa kwa sekta binafsi ikiongezeka kwa asilimia 9.1 ndani ya mwaka mmoja uliopita, sehemu kubwa ya mikopo hiyo imekuwa ikiwanufaisha zaidi watu binafsi ambao wanamiliki shughuli mbalimbali za uzalishaji ikiwemo biashara.
Ripoti ya Tathmini ya Uchumi ya mwezi Februari 2020 (Economic Monthly Review) iliyotolewa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) hivi karibuni inaeleza kuwa mikopo kwa sekta binafsi imeongezeka kwa wastani wa asilimia 9.1 katika mwaka ulioishia Januari 2020 ikilinganishwa na asilimia 7.3 iliyorekidiwa katika kipindi kama hicho mwaka 2019.
“Kuongezeka kwa kasi ya ukuaji wa mikopo hiyo kulichangiwa na usimamizi thabiti wa sera ya fedha, ongezeko la shughuli za kiuchumi na jitihada zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali za kuboresha mazingira ya biashara,” inasomeka sehemu ya ripoti hiyo inayopatikana pia katika tovuti ya BoT.
Ripoti hiyo inaeleza kuwa sehemu kubwa ya mikopo kwa sekta binafsi imeendelea kuelekezwa kwa watu binafsi au kaya ambazo zilipata wastani wa asilimia 29.6 ya mikopo yote ikifuatiwa na shughuli za biashara zilizokuwa na wastani wa asilimia 17.9.
Sekta nyingine zilizonufaika na mikopo hiyo ni pamoja na ujenzi, kilimo, usafirishaji na mawasiliano, madini, hoteli na migahawa.
Soma zaidi:
- Serikali yaanika bajeti ya mwaka 2019/2020
- Serikali yasema ongezeko la bajeti ya kilimo litategemea mahitaji ya kibajeti ya sekta nyingine
- Kasi ya ukopeshaji sekta binafsi yapaa mara tatu
Mikopo inayoelekezwa katika shughuli zote kubwa za uchumi imeendelea kuongezeka, isipokuwa kwa shughuli za hoteli na migahawa ambayo ilishuka kwa asilimia 10.3 katika kipindi hicho.
Hata wakati mikopo kwa sekta binafsi ikiongezeka, riba zinazotozwa na benki za biashara nayo imeshuka, jambo ambalo ni kiasharia kizuri kwa ukuaji wa sekta ya fedha na uchumi,
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, riba iliyotozwa kwenye mikopo iliyotolewa na benki ilikuwa wastani wa asilimia 16.7 mwezi Januari 2020 ikishuka kutoka wastani wa asilimia 17.3 katika kipindi kama hicho 2018.
Benki kutoza riba ndogo, kunatoa fursa kwa wananchi wengi zaidi wakiwemo wakulima na wafanyabiashara kunufaika na mikopo inayotolewa na taasisi hizo za fedha kwa ajili ya kujiletea maendeleo yao.