Bei ya petroli,dizeli yashuka kiduchu Tanzania
- Petroli yashuka kwa Sh7 na dizeli kwa Sh74.
- Ewura waeleza sababu za kushuka kwa bei ya mafuta.
Dar es Salaam. Huenda watumiaji wa wa vyombo vya moto wakashusha pumzi kidogo mara baada ya bei ya petroli na dizeli kushuka kiduchu, ikichangiwa na kupungua kwa bei ya mafuta katika soko la dunia.
Bei ya mafuta nchini imekuwa ikipanda mfululizo kuanzia mwezi Julai hali inayoacha maumivu kwa watumiaji wa vyombo vya moto nchini.
Kwa mujibu wa taarifa ya Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) ya bei mpya za mafuta zinazoanza kutumika leo Novemba1, 2023, lita moja ya petroli Jijini Dar es Salaam imeuzwa kwa Sh3,274 ukilinganisha na Sh3,281 iliyokuwa ikitumika mwezi Oktoba mwaka huu.
Ahueni hiyo katika bei ya mafuta ya petroli ni ya Sh 7 tu ambayo ni kwa mafuta yaayoingia nchini kupitia bandari ya Dar es Salaam.
Bei ya mafuta ya dizeli nayo imeshuka kwa Sh 74 kutoka Sh3,448 iliyokuwa ikitumika mwezi Oktoba hadi Sh3,374 inayoanza kutumika leo.
Soma zaidi:Tanzania, Ujerumani kuanza mazungumzo kurejesha mabaki ya miili na mafuvu
Uchambuzi zaidi wa bei hizo unaonyesha kuwa licha ya bei hizo kushuka bado watumiaji wa vyombo vya moto watendelea kutoboa mifuko yao kuipata huduma hiyo.
Kama ulikuwa unatumia Sh10,000 kupata lita 3 za petrolii na lita 2 za dizeli kwa bei mpya zilizotolewa leo bado fedha hiyo itanunua kiwango kile kile cha mafuta.
Wakati watumiaji wa mafuta mkoani Dar es Salaam wakitoboa mifuko kupata mafuta, wakazi wa Kyerwa(Ruberwa) wananunua petroli kwa Sh3,512 na dizeli kwa Sh3,612 ikiwa ni bei ya juu zaidi kuliko sehemu nyingine nchini.
Bofya hapa kuona bei za mafuta mwezi Novemba nchi nzima
Sababu za kushuka kwa bei ya mafuta zatajwa
Ewura inasema kushuka kwa bei ya mafuta kwa mwezi Novemba nkumechanguwa na sababu mbalimbali ikiwemo kushuka kwa bei ya mafuta katika soko la dunia
“Mabadiliko ya bei za mafuta kwa mwezi Oktoba 2023 yanatokana na kupungua kwa bei za mafuta katika soko la dunia kwa wastani wa asilimia 5.68 na gharama za uagizaji wa mafuta kwa wastani wa asilimia 13 kwa petroli…
…Asilimia 25 kwa dizeli na uamuzi wa wazalishaji wakubwa wa mafuta duniani (OPEC) kupunguza uzalishaji na vikwazo vya kiuchumi ambavyo nchi ya Urusi imewekewa na mataifa ya magharibi,” imeainisha taarifa ya Ewura.
OPEC ina wanachama 13 ikiwemo Saudi Arabia na washirika wake 10 wakiongozwa na Urusi ambapo Julai 2023 waliazimia kupunguza uzalishaji wa mafuta ili kuongeza thamani ya bidhaa hiyo muhimu duniani.