Bajeti ya Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji 2026/27 yashuka kwa asilimia 3.6
- Matumizi ya kawaida yaongezeka kwa asilimia 33, matumizi ya miradi ya maendeleo yapungua kwa asilimia 5.84.
Dar es Salaam. Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji imeliomba Bunge liidhinishe bajeti ya Sh144.85 bilioni kwa mwaka wa fedha 2026/27, huku sehemu kubwa ya fedha hizo ikielekezwa kwenye matumizi ya kawaida.
Prof Kitila Mkumbo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji aliyekuwa akiwasilisha bajeti hiyo leo Aprili 16, 2026 bungeni jijini Dodoma amesema kati ya fedha hizo, Sh126.02 bilioni zitatumika kwa matumizi ya kawaida na Sh18.83 bilioni kwa miradi ya maendeleo.
“Ofisi Rais, Mipango na Uwekezaji na taasisi zilizo chini yake inaliomba Bunge lako tukufu lipokee, lijadili na kuidhinisha jumla ya Sh144.8 bilioni ikiwa Sh126 bilioni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Sh18.83 bilioni kwa ajili ya miradi ya maendeleo kwa mwaka 2026/27,” amesema Prof Mkumbo.
Bajeti hiyo imepungua kwa Sh3 bilioni sawa na punguzo la asilimia 3.6 ukilinganisha na Sh148.62 bilioni iliyoidhinishwa mwaka wa fedha 2025/2026 ikichangiwa na matumizi ya kawaida kupungua.
Asilimia 87 ya bajeti hiyo imeleekezwa katika matumizi ya kawaida ya wizara hiyo yanayohusisha gharama za uendeshaji wa ofisi, posho na mishahara ya watumishihuku asilimia 13 iliyobakia ikitengwa kwa ajili ya shughuli za maendeleo.
Katika mgawanyo wa fedha hizo, kiasi cha Sh22.42 bilioni kimetengwa kwa ajili ya mishahara, huku Sh103.6 bilioni zikitengwa kwa matumizi mengineyo ya kawaida.
Fedha za matumizi ya kawaida zimeongezeka kwa asilimia 3.19 kutoka Sh122.12 bilioni hadi Sh126.02 bilioni Ikilinganishwa na mwaka wa fedha 2025/26.
Kwa upande wa miradi ya maendeleo, bajeti imepungua kwa asilimia 28.96. kutoka Sh26.50 bilioni hadi Sh18.83 bilioni.
Zena Maulid Katambo, aliyemwakilisha Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, amesema kuwa punguzo la bajeti hiyo limetokana na kupungua kwa fedha za maendeleo.
Aidha, Katambo amesema kucheleweshwa kwa fedha za maendeleo kunasababisha miradi ya Serikali kushindwa kukamilika kwa wakati, hivyo kuiomba Serikali kuhakikisha fedha hizo zinatolewa kwa ukamilifu na kwa wakati.

Maeneo ya vipaumbele kwa mwaka wa fedha 2025/26
Katika mwaka ujao wa fedha Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji inalenga kuratibu maandalizi ya mpango wa maendeleo wa Taifa wa miaka mitano, kwa kuzingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.
Aidha, itaendelea kufuatilia utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya Taifa, kufuatilia utekelezaji wa maeneo muhimu ya vipaumbele vya Taifa, kutathmini rasilimali za nchi, kuwezesha na kutoa huduma kwa wawekezaji wa sekta binafsi.
Vipaumbele vingine ni kuimarisha uwekezaji wa umma na kuimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji.
Kwa upande wa taasisi zilizo chini ya wizara, tume ya Taifa ya mipango itasimamia tathmini ya miradi ya kimkakati, kuendesha tafiti za kuboresha upangaji wa maendeleo, na kuandaa miongozo ya utekelezaji wa dira ya Taifa ya maendeleo 2050.
Latest