Ahueni Serikali ya Tanzania ikipunguza ada ya ving’amuzi

June 28, 2022 10:57 am · David
Share
Tweet
Copy Link
  • Awali ilikuwa Sh1,000 hadi Sh3,000 na sasa Serikali inasema itatoza ada ya kati ya Sh500 hadi Sh2,000 kadri ya matumizi. 
  • Ni baada ya wananchi kulalamika kiwango kilichopendekezwa wiki mbili zilizopita. 

Dar es Salaam. Baada ya kuwepo malalamiko lukuki kutoka kwa wananchi na wadau juu ya pendekezo la ada ya ving’amuzi, Serikali imeamua kupunguza ada hiyo kwa kiwango cha kati ya Sh500 na Sh1,000.

Awali Serikali ilipendekeza wananchi wote wanaotumia huduma ya ving’amuzi watozwe kiasi cha Sh1,000 hadi Sh3,000 kulingana na matumizi lakini katika maboresho ya bajeti kuu ya Serikali ya mwaka 2022/23 sasa ada hiyo itakuwa kati Sh500 hadi Sh2,000. 

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, Daniel Sillo aliliambia Bunge jijini Dodoma Juni 27, 2022 wakati akitoa maoni ya kamati juu ya Muswada wa Sheria ya Fedha 2022 kuwa Serikali imekubali kupunguza ada hiyo.

“Serikali ilileta mapendekezo ya kutoza kuanzisha tozo ya Sh1,000 hadi Sh3,000 kwa ving’amuzi itakayokuwa ikitozwa kupitia malipo ya king’amuzi hata hivyo baada ya majadiliano ya kina ilionekana kwamba kiwango hicho ni kikubwa,” amesema Mbunge Sillo.

Baada ya majadiliano hayo, Sillo amesema Serikali imeridhia kiwango cha Sh500 hadi Sh2,000 kitozwe wa watumiaji wa ving’amuzi.

Ndani ya majuma mawili, baadhi ya wananchi wamekuwa wakipinga pendekezo la Serikali la kutoza ada ya kati ya Sh1,000 hadi Sh3,000 kwenye ving’amuzi kutokana na matumizi wakieleza kuwa uamuzi huo utaongeza gharama za maisha na kuminya uhuru wa kupata habari.


Soma zaidi


Daniel Mdeka, mkazi wa Mwananyamala jijini Dar es Salaam amesema Serikali inaonekana kukosa ubunifu wa kukusanya mapato kwa kuwa kwa sasa inaweza kutafuta vyanzo vingine vya pesa kuliko kuongeza tozo ambazo zinazidi kumwongezea mwananchi makali ya maisha.  

Uamuzi huo wa sasa wa Serikali utapunguza kidogo maumivu kwa watumiaji wa ving’amuzi ambavyo ni muhimu katika upashanaji habari na burudani nchini. 

Hadi mwaka 2021, takwimu za Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) zinabainisha kuwa kulikuwa na ving’amuzi hai milioni 3.19 ambavyo kati yake milioni 1.58 vinatumia satelaiti.

Iwapo Serikali itatoza ada angalau Sh500 kwa kila king’amuzi huenda ikavuna Sh1.59 bilioni kwa mwezi kutoka kwenye vifaa hivyo hai sawa na Sh19.08 bilioni kwa mwaka.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW