Si kweli: Madoa meusi kwenye nyayo huashiria maambukizi ya VVU
- Wataalam wathibitisha, njia pekee ya kutambua maambukizi ni kufanyiwa vipimo na daktari, matabibu wa ngozi watoa sababu.
Dar es Salaam. Katika siku za hivi karibuni, mitandao ya kijamii imefurika madai yanayodai kuwa mtu mwenye madoa meusi kwenye nyayo za miguu anaishi na Virusi vya Ukimwi (VVU). Madai ambayo si ya kweli.
Madai hayo yameenea kupitia mitandao ya kijamii hususan Facebook, Instagram na TikTok, yakichochewa zaidi na mjadala ulioibuka baada ya mtengenezaji wa maudhui anayefahamika kwa jina la Cherry Hollister kumtuhumu mtengenezaji mwingine wa maudhui kwa jina la Dotto Magari kuwa anaishi na VVU na kuwataka wananchi kutafsiri madoa yaliyopo kwenye nyayo zake kama ushahidi wa maambukizi.
Hata hivyo, uchunguzi uliofanywa na Nukta Fakti umebaini kuwa madai hayo hayana msingi wa kitabibu.
Kwa kufanya mazungumzo na wataalamu wa afya na matabibu Nukta Fakti imejiridhisha kuwa hakuna uhusiano wowote uliopo, kati ya madoa meusi kwenye nyayo na maambukizi ya VVU.
Ukweli ni huu
Daktari wa binadamu kutoka mkoani Sumbawanga, Dk Lameck Swax ameithibitishia Nukta Fakti kuwa si kweli kwamba mtu mwenye madoa meusi kwenye nyayo basi ana VVU.
Dk Swax anaeleza kuwa njia pekee inayoweza kuthibitisha kuwa mtu anamaambukizi ni vipimo kutoka kwa daktari na si madoa meusi kwenye nyayo
Ameongeza kuwa mara nyingi madoa kwenye nyayo husababishwa na mambo mengine ikiwemo kiwango cha melanin, na rangi asili ya ngozi, na si maambukizi ya VVU.
“Melanini inaweza kuonekana hata kwenye nyayo za miguu, lakini hilo si kiashiria kwamba mtu ana VVU,” anaeleza mtaalamu huyo.
Kwa upande wake, mtaalamu wa maabara kutoka Hospitali ya Wilaya ya Mafia iliyopo mkoani Pwani, Frank Zefania ameiambia Nukta Fakti kuwa licha ya uzoefu alionao katika kufanya vipimo, VVU haijawahi kuthibitika kwa kumuangalia mtu kwa nje.
“Ni lazima ufanye vipimo kwa kuchukua sampo ya damu na kuichunguza ndipo tujue, pamoja na uzoefu wangu kwenye kufanya vipimo siwezi kumtambua maambukizi ya VVU kwa kumuangalia mtu,” amesema Zefania.
Chanzo cha madoa meusi ni hiki
Daktari wa magonjwa ya ngozi, Dk Nuru Malema kutoka mkoani Nzega ameiambia Nukta Fakti kuwa watu hupata madoa kwenye nyayo kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo mzio ambao kitaalamu unajulikana kama ‘Papular Urticaria’
Dk Malema ameongeza kuwa madoa meusi pia yanaweza kusababishwa na mlipuko wa vipele vinavyowasha ‘Pruritic Papular Eruption (PPE). Licha ya kuwa mtu yeyote anaweza kupata maambukizi, amebainisha kuwa madoa hayatoki unyayoni pekee.
“Hali hiyo husababisha vipele vinavyoweza kutokea sehemu mbalimbali za mwili na si kwenye nyayo pekee, hivyo haiwezi kutumika kama kipimo cha kubaini maambukizi ya VVU,” amethibitisha Dk Malema.
Ushahidi wa kisayansi unasemaje?
Tafiti zinaonyesha kuwa watu wanaoishi na VVU wanaweza kupata matatizo mbalimbali ya ngozi, lakini matatizo hayo hutokea kutokana na kupungua kwa kinga ya mwili, si kwa sababu ya kuwepo kwa madoa meusi kwenye nyayo za miguu.
Tovuti ya masuala ya afya ya WebMD yenye makao makuu yake Marekani inaeleza kuwa, baadhi ya magonjwa ya ngozi yanayoweza kuonekana kwa watu wenye VVU ni pamoja ‘kaposi sarcoma’, ‘Pruritic Papular Eruption (PPE)’, ‘herpes’, ‘thrush’ na ‘photodermatitis’
Hata hivyo, hakuna hata moja kati ya hali hizo inayotambuliwa kitabibu kuwa ni madoa meusi kwenye nyayo za miguu yanayoweza kutumika kuthibitisha mtu anaishi na VVU.