Wanawake wanavyoweza kujenga afya ya akili kazini
- Kujisamehe na kujenga utulivu wa ndani ni tiba muhimu kwa afya ya akili.
- Vikundi vya msaada na ushauri wa kitaalamu vyapewa kipaumbele.
Dar es Salaam. Kuna wakati msongo wa mawazo au sonona vinavyopowakabili wanawake kutokana na presha za kikazi, kimaisha na familia, wengi hukata tamaa bila kusaka suluhu.
Habari njema ni kwamba wanaweza kufanya kazi zao vizuri kazini huku wakilinda afya yao ya akili iwapo watafuata ushauri wa wataalamu wa afya.
Katika makala iliyopita tuliona namna baadhi ya wanawake wanaokabiliwa na changamoto za afya ya akili kutokana na kuendelea kuwa tegemeo kazini, katika familia na jamii, presha ambayo ni kubwa kuliko wanaume. Hali hiyo imewasababisha msongo wa mawazo au wengine kufikia kupata sonona kwa muda mrefu.
Ili kukabiliana na hali hiyo, wanasaikolojia wanashauri kuepuka mazingira au watu wanaochochea maudhi kama njia moja wapo ya kujinga na changamoto ya afya ya akili.
Tafuta msaada
Changamoto hii mara nyingi huchochewa na ukosefu wa msaada kutoka kwa wenzake au uongozi wa mabavu, ukatili, unyanyasaji au uonevu kazini, ubaguzi na kutengwa ama kukosa usalama wa ajira, malipo duni au uwekezaji hafifu katika maendeleo ya taaluma.
Kwa mujibu wa daktari bingwa wa magonjwa ya afya ya akili Silvia Ngonyani kutoka hospitali ya wilaya ya Kisarawe, wanawake wanaweza kuimarisha afya yao ya akili kazini kwa kuchukua hatua za makusudi za kujilinda na kujijenga kisaikolojia.

Si lazima uwe na fedha nyingi
Dk Ngonyani anasema kuwa si kila suluhisho linahitaji fedha nyingi kwa kuwa kuna mambo yanayoweza kufanywa na mtu binafsi na kuleta matokeo chanya.
Miongoni mwa hatua hizo ni kuepuka mazingira au watu wanaochochea maudhi, kujifunza mbinu za kudhibiti msongo wa mawazo (stress management) kama kupanga ratiba vizuri, kupumzika, kufanya mazoezi na kutafakari.

Tafuta ushauri wa mwanasaikolojia
Iwapo bado mambo hayaendi, Dk Ngonyani anashauri utafute ushauri wa kitaalamu kutoka kwa mwanasaikolojia ili kupata mwongozo sahihi wa namna ya kukabiliana na changamoto.
“Dawa pekee haitoshi kutibu changamoto za afya ya akili. Ni muhimu mtu akapata ushauri wa kitaalamu, ajisamehe pale alipojikwaa, na ajenge amani ya ndani ili aweze kuendelea na maisha kwa utulivu,” anasema daktari huyo aliyetibu mamia ya wagonjwa wenye changamoto ya afya ya akili.

Jenga utulivu wa ndani
Vilevile, wataalamu wanashauri kujenga utulivu wa ndani kupitia imani ya kiroho kwa kusali, kutafakari, kushukuru na kuomba amani ya moyo ili kuimarisha afya ya akili.
Ingawa si rahisi kumiliki au kukubali tukio lililoumiza, kutafuta amani ya ndani humwezesha mtu kupata nguvu ya kuendelea mbele badala ya kubaki katika maumivu ya muda mrefu.
Jifunze kusema hapana
Ukiachana na mbinu za kitabibu, Leyla Abubakri, Mtaalamu wa saikolojia na mahusiano kutoka mkoani Tanga anashauri wanawake kujenga uwezo wa kuweka mipaka (personal boundaries) mahali pa kazi na nyumbani.
Hii inahusisha kujifunza kusema “hapana” pale majukumu yanapozidi uwezo, kuepuka kubeba kila jukumu peke yao, na kutambua kuwa kujilinda si ubinafsi bali ni kujithamini.

Jenga mtandao wa kukulinda
Kujenga mtandao wa kijamii wa kuaminika (support system) unaojumuisha marafiki, familia au wenzake wa kazi wanaoweza kusikiliza bila kuhukumu.
Kwa Leyla, kuzungumza na mtu sahihi hupunguza mzigo wa mawazo kwa kiasi kikubwa na kuimarisha ustahimilivu wa kihisia.
Kujijengea utambulisho binafsi nje ya kazi na majukumu ya kifamilia, Leyla anasema wanawake wengi hujifunga katika majukumu ya kuwa mama, mke au mfanyakazi na kusahau wao ni nani binafsi.
Tenga muda wa kujifunza mambo mapya
Mtaalamu huyo anashauri kutenga muda wa kujifunza jambo jipya, kuwa na kitu ambacho mtu atapendelea kukifanya (hobbies) au shughuli inayompa mtu furaha binafsi ili kurejesha nguvu ya ndani.
Wanawake wanapaswa kujifunza kutambua mapema dalili za uchovu wa kihisia, anasitiza Leyla, kama kukosa hamasa ya kazi, hasira za mara kwa mara au kujitenga na wengine, na kuchukua hatua kabla hali haijawa kubwa.
Kwa kufanya hivyo, wanaweza kudhibiti changamoto za afya ya akili kabla hazijaathiri utendaji na maisha yao kwa ujumla.
Kwa ujumla, kuimarisha afya ya akili makazini kunahitaji utayari wa mtu binafsi, msaada wa kitaalamu na mazingira yanayoruhusu mazungumzo ya wazi bila hofu wala unyanyapaa.