Balozi Kombo avunja ukimya suala la Polepole
- Adai ameiona barua ya Polepole mtandaoni kama wengine walivyoiona.
- Asema ufafanuzi utawekwa bayana taratibu zitakapo kamilika.
Dar es salaam. Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wa Tanzania, Balozi Mahmoud Thabit Kombo amesema taarifa kuhusu Balozi Humphrey Polepole zitatolewa na mamlaka husika zitakapokamilisha taratibu.
Balozi polepole aliandika barua yake ya kujiuzulu Julai 13, 2025 kwenda kwa Rais Samia akitaja sababu ni kutoridhishwa na mwelekeo wa uongozi usiojielekeza katika kusimamia haki, amani na kuheshimu watu ambapo tangu wakati huo hakuna kiongozi yeyote wa Serikali aliyejitokeza kutoa majibu.
Balozi Kombo aliyekuwa akizungumza na wanahabari leo, Julai 23, jijini Dar es Salaam, kuhusu mkutano wake na mawaziri pamoja na maofisa waandamizi wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), amesema hata yeye ameona taarifa hizo kupitia mitandao ya kijamii, kama walivyoona wananchi wengine.
Waziri huyo wa Mambo ya Nje ameeleza kuwa pamoja kuona barua hiyo kwenye mtandao, barua hiyo haikuelekezwa kwake hivyo ni ngumu kusema lolote badala yake mamlaka iliyoelekezewa barua hiyo ndiyo yenye nafasi ya kutolea ufafanuzi.
“Kama juu ingekuwa imeandikwa Mahmoud Thabit Kombo, Waziri wa mambo ya Nje ningeweza kutolea ufafanuzi,” amesema Balozi Kombo.
Hata hivyo, Balozi Kombo amesema suala la kiongozi huyo linahusisha sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma na anaamini kuwa taratibu zitakapokamilika zitatolewa taarifa.
“Suala lile lina masuala ya kisheria, kanuni na utumishi wa umma na lina taratibu zake zikikamilika kwa utumishi wa umma taarifa za kina zitatolewa,” ameongeza Balozi Kombo.
Latest