Balozi Polepole kupigwa msasa kabla ya kwenda Malawi

March 15, 2022 10:48 am · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link

Rais  wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan akimuapisha Humphrey Polepole kuwa Balozi wa Tanzania katika nchi ya Jamhuri ya Malawi kwenye hafla fupi iliyofanyika Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma leo Machi 15, 2022. Picha | Ikulu.


  • Ameapishwa leo baada ya kuteuliwa jana kuwa Balozi nchini Malawi.
  • Kabla ya kwenda Malawi atapewa darasa katika  Chuo Cha Diplomasia.
  • Atakutana na kuzungumza na Rais Samia. 

Dar es Salaam. Baada aliyekuwa Mbunge wa kuteuliwa Humphrey Polepole kuapa leo kuwa Balozi wa Tanzania nchini Malawi anatarajia “kupigwa msasa” katika  Chuo Cha Diplomasia jijini Dar es Salaam kabla ya kuanza majukumu yake mapya.

Polepole ambaye aliwahi kuwa Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) aliteuliwa jana Machi 14, 2022 kuwa Balozi na kuachia nafasi yake ya ubunge wa Bunge la Tanzania. 

Rais Samia Suluhu Hassan aliyekuwa akishuhudia Polepole akiapa leo Machi 15, Ikulu, Dodoma amesema Balozi huyo atapelekwa katika Chuo Cha Diplomasia ili kupewa darasa kabla ya kuanza majukumu yake.

“Mheshimiwa Balozi najua baada ya hapa watakuweka darasani kwanza pale Chuo Cha Diplomasia,” amesema Rais Samia.

Kiongozi huyo mkuu wa nchi amemwambia Polepole kuwa, “utakapotoka pale kabla hujaenda Malawi nitakutana nawe kwa hiyo tutazungumza kwa urefu.”


Soma zaidi:


Aidha, Rais Samia amemuagiza Mkuu wa Mkoa mpya wa Njombe, Waziri Kindamba aliyeapa leo kuendeleza kazi nzuri iliyofanywa na mtangulizi wake kwa kuhakikisha mkoa huo unainuka kiuchumi kwa sababu una fursa nyingi.

“Njombe una kila kitu, kama utatulia unaweza ukapandisha kipato kwa kiasi kikubwa. Lakini kuna mambo mengi ya kuangalia pamoja na kwamba Njombe ni mkoa unaozalisha chakula kwa wingi tuna changamoto ya nuktrition (lishe) kaangalie vizuri,” amesema Rais Samia. 

Kindamba aliteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Njombe akichukua nafasi ya Mhandisi Marwa Rubirya anayestaafu.

Amemuagiza pia kuongeza hamasa kwa watu kupata chanjo kwa sababu bado Corona ipo na kuna uwezekano aina mpya ya kirusi cha Omicron ikajitokeza duniani. 

“Usisahau suala la chanjo. Nenda jitahidi kashirikiane na wenzako kahamasishe watu wachanje kama mlivyosikia tayari kuna Omicron B01 ameanza huko Asia. Na wakianza huko, hawako mbali kuja kwetu, naomba mkasimamie hili,” amesisitiza Rais. 

Kabla ya uteuzi huo, Kindamba alikuwa  Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) ambapo nafasi yake imechukuliwa na Peter Ulanga.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW