Sh1.5 trilioni zahitajika kutokomeza virusi vya Corona
- WHO yasema fedha hizo zitatumika katika maandalizi na kukabiliana na mlipuko huo wa Corona.
- Idadi ya vifo kutokana na homa hiyo inakaribia watu 500.
Dar es Salaam. Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Dk Tedross Adhamon Ghebreyesus, ametoa ombi la dola za Marekani milioni 675 ili kuongeza nguvu juhudi za kimataifa za kukabiliana na mlipuko wa virusi vipya vya Corona wakati idadi ya vifo kutokana na homa hiyo ikikaribia watu 500.
Kiasi hicho pesa ambacho ni sawa na takriban Sh1.5 trilioni kitasaidia katika ununuzi wa vifaa, mafunzo kwa wahudumu na kudhibiti kusambaa kwa ugonjwa huo katika maeneo mengine.
Akizungumza mjini Geneva, Uswis jana (Februari 5, 2020) Dk Ghebreyesus amesema takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kuwa kuna visa 4,363 vilivyothibitishwa nchini China na vifo 490 tangu kutangazwa kwa mlipuko huo Desemba 31 mwaka jana.
“Katika saa 24 zilizopita tumekuwa na visa vingi zaidi katika siku moja tangu kuzuka kwa mlipuko huo. Tusisahau ni jinsi gani ilivyo vigumu kwa watu wa Wuhan, hivyo kufanya kila liwezekanalo katika sehemu ambayo ni kitovu cha mlipuko huo itasaidia kupunguza kasi ya kusambaa kwa virusi hivyo na hilo ndilo tunalolishuhudia,” amesema Ghebreyesus katika taarifa ya Umoja wa Mataifa (UN).
WHO imeeleza kuwa nje ya China kumeripotiwa visa 191 hadi sasa katika nchi 24 na kumekuwa na kifo kimoja nchini Ufilipino.
Kati ya visa hivyo, visa 31 havina historia yoyote ya kusafiri kwenda China lakini vyote vina uhusiano wa karibu na visa vilivyothibitishwa au mtu aliyetoka kwenye mji ulikoanzia mlipuko huo wa Wuhan.
Soma zaidi:
- Watanzania waishio China watolewa hofu virusi vya corona
- Picha, sauti ya uzushi virusi vya corona zinavyojipenyeza mtandaoni Tanzania
- Mikakati ya Tanzania kukabiliana na virusi vya Corona
Hatua zilizochukulia mpaka sasa
Dkt Tedross amesema WHO imetoa dola milioni 9 (Sh20.7 bilioni) kutoka kwenye mfuko wake wa ufadhili wa dharura ili kusaidia kukabiliana na mlipuko huo.
Pia amesema WHO imesambaza vifaa 500,000 vya kujikinga na maambukizi pamoja na glovu 350,000, vifaa vya kupumua 40,0000 na mavazi ya wagonjwa 18,000 kwa nchi 24.
Shirika la afya pia limepeleka vipimo 250,000 kwenye maabara zaidi ya 70 kote duniani ili kuharakisha upimaji wa virusi hivyo.
”Lakini tunahitaji kufanya zaidi” amesema Ghebreyesus kabla ya kuainisha fedha hizo dola milioni 675 zitakavyotumika katika maandalizi na kukabiliana na mlipuko huo wa Corona.
“Tunatambua kwamba watu wanahofu na wasiwasi na ni sawa kuwa hivyo, lakini huu sio wakati wa kuogopa, huu sio wakati wa taharuki, ni wakati wa kuchukua hatua kutokana na ushahidi na uwekezaji wakati bado tukiwa na fursa ya kuweza kuudhibiti mlipuko huu,” amesisitiza bosi huyo wa WHO.
Hadi sasa hakuna dawa iliyothibitika kutibu virusi vya Corona. Hivyo wito wa hatua za haraka na za pamoja unaweza kushughulikia hatari hizo kwa mujibu wa WHO na maeneo mengine yanayohitaji msaada.
Latest