Wakulima zaidi ya 7,000 kunufaika kilimo cha mboga, matunda Tanzania
- Ni mradi utakaowanufaisha wakulima 7,500 wa mikoa mitatu ya Mbeya, Songwe na Katavi.
- Watawezeshwa kulima kwa kisasa mazao ya mboga mbaga na matunda ili kupata masoko ya uhakika.
- Pia utaongeza usalama wa chakula na lishe.
Mbeya. Wakulima wa mboga mboga na matunda wa Nyanda za Juu Kusini nchini Tanzania, sasa wana kila sababu ya kutabasamu kwa sababu wana uhakika wa kuongeza uzalisahaji na masoko ya mazao yao.
Wakulima 7,500 wa mikoa mitatu ya Mbeya, Songwe na Katavi watanufaika na mradi wa mboga mboga na matunda ili kuongeza tija ya uzalishaji, upatikanaji, usalama wa chakula pamoja na kuboresha hali ya lishe katika ukanda huo.
Mkurugenzi wa programu ya mboga mboga na matunda wa shirika la Helvetas, Nyanda za Juu Kusini linalosimamia mradi huo, Daniel Kalimbiya amesema mradi huo ni wa miaka minne ambapo imeanza mwaka huu na utakamilika mwaka 2024 ambapo vikundi vya wakulima 500 pamoja na vyama vya ushirika vinavyojihusisha na kilimo hicho vitanufaika.
“Mradi huu wa miaka minne ambao ulianza Mei 2020 hadi kukamilika kwake utawafikia wakulima wa mboga mboga na matunda wapatao 7,500 kutoka kaya 1,500 ili kuongeza tija na thamani kwenye mazao hayo.
“Sambamba na ujenzi wa viwanda ili kusaidia usindikaji kwa sababu mazao mengi yanapotea licha ya kuyahifadhi lakini pia kuwatafutia masoko na kutoa elimu ya uzalishaji bora ili kukidhi viwango vinavyohitajika, kitaifa na kimataifa,” amesema Kalimbiya wakati wa warsha ya wadau wa kilimo iliyofanyika hivi karibuni mkoani Mbeya.
Mradi huo utasaidia kuinua na kuboresha maisha wakulima wanawake na vijana ambao ndiyo nguvukazi kubwa katika sekta ya kilimo.
Zinazohusiana
- Biashara ya juisi inavyowatoa kimaisha wasomi waliokataa kuajiriwa
- Idrisa Magesa: Kijana aliyerithi mikoba ya kuuza uji kutoka kwa bibi yake
- Mambo ya kuzingatia unapoanzisha brand yako ya biashara
Katibu Tawala Mkoa wa Mbeya Idara ya Uchumi na Uwekezaji, Said Madito amesema shirika linapaswa kuongeza thamani ya mnyororo wote mazao kwa kuhakikisha uzalishaji wa kilimo hicho unafanikiwa ili kuleta matokeo chanya badala ya kuishia njiani.
Aidha, ameshauri shirika hilo kufanya tathmini na ufuatiliaji wa mradi huo ili kutambua matokeo ya kile walichokifanya kwa kipindi cha miaka hiyo minne.
”Nawapongeza shirika kwa kuamua kuwasaidia wakulima wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, sekta ya mboga mboga na matunda ilikuwa nyuma kwa sababu wakulima wanakabiliwa na ukosefu wa mitaji ili kuzalisha lakini pia hakuna uwekezaji mkubwa ukilinganisha na ukanda wa kaskazini sambamba na ukosefu wa taarifa sahihi za uzalishaji,” amesema Madito.
Mkurugenzi wa Kituo cha Utafiti wa Kilimo (Tari) tawi la Uyole jijini Mbeya Dk Tulole Bucheyeki amesema shirika la Helvetas kwa kushirikiana na kituo hicho, watahakikisha wanawanufaisha wakulima kwa kuwapa elimu, kuwatafutia masoko na kuwajengea viwanda vya usindikaji.
Amesema katika mradi huo utaweza kuwanufaisha wananchi milioni 1 ingawa sio moja kwa moja kupitia usambazaji wa pembejeo za kilimo, wauzaji na walaji wa mazao au bidhaa zitakazozalishwa.
“Kituo cha Tari-Uyole katika program hiyo kimejikita katika kushauri aina ya mbegu zinazofaa kutumika, lishe kwa kutoa ushauri wa aina gani ya chakula kinachofaa kutumiwa pamoja na matumizi bora ya pembejeo za kilimo,”anasema Dk. Bucheyeki.
Ofisa Kilimo Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Merius Nzalawahe, anayeshughulikia mazao ya bustani, anasema mazao hayo, yana faida kubwa kwa sababu yanatumia eneo dogo lakini mavuno yanakuwa mengi ukilinganisha na mengine hivyo amewahimiza wakulima kujikita katika eneo hilo.
Amesema Serikali inaendelea na jitihada zake za kuhamasisha kilimo cha mboga na matunda kwa kuwahimiza waendelee kuongeza maeneo kwa ajili ya uzalishaji wa kilimo hicho.
Hata hivyo, amewataka wakulima kufuata ushauri unaotolewa na wataalam wa kilimo ili kongeza tija katika uzalishaji na ubora ili kupunguza upotevu wa mazao wakati wa kuvuna.