Wakulima wa pamba Mwanza wapewa mbinu mpya kuongeza uzalishaji
- Ni pamoja na kuzingatia kanuni za kilimo na kutumia pembejeo kwa usahihi.
- Wakulima waonywa kutochanganya pamba na mazao mengine katika shamba moja ili kuepuka wadudu.
Mwanza. Huenda wakulima wa pamba mkoani Mwanza wakaanza kuzalisha zao hilo kwa tija na kuongeza kipato chao mara baada ya kupatiwa mafunzo ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara.
Pamba ni miongoni mwa mazao muhimu kwa uchumi wa Tanzania kwa kuwa linatoa ajira kwa takriban asilimia 40 ya Watanzania wote katika mnyororo wa thamani ambapo kwa mujibu wa Bodi ya Pamba Tanzania (TCB) zao hilo linalimwa takribani mikoa 17 na wilaya 56.
Balozi wa pamba nchini, Agrey Mwanri aliyekuwa ziarani katika vijiji vya Lubili, Ilalambogo na Isenegeja wilayani Misungwi, kwa dhumuni ya kutoa elimu ya zao hilo amebainisha kuwa kutofuata kanuni bora za kilimo ni miongoni mwa sababu inayofanya wakulima kupata mavuno hafifu ya pamba.
“Kilimo cha pamba kimekuwa kikipitia nyakati mbalimbali, zamani wakulima walilima bila kufuata kanuni na hawakuwa wanatumia mbolea na viatilifu hali ambayo ilisababisha uzalishaji kuwa mdogo, kutokana na tafiti mbalimbali watalaamu wamekuja na mbinu mbadala zitakazosaidia katika uzalishaji,” amesema Mwanri.
Soma zaidi : TCU yafungua dirisha la nne udahili elimu ya juu 2023-2024
Miongoni mwa kanuni za kilimo bora cha pamba zinazopendekezwa na wataalamu ni pamoja na kupanda kwa kutumia vipimo sahihi ili kuyapa nafasi mazao kustawi bila kubanana, kuweka mbolea kwa kuzingatia kipimo pamoja na kunyunyiza dawa ya wadudu kwa usahihi.
Mbinu nyingine iliyonainishwa ni kutochanganya zao la pamba na mazao mengine ya chakula ndani ya shamba moja kwa kuwa kitendo hicho husababisha uwepo kwa wadudu wanaoshambulia zao hilo.
Kwa mujibu wa Afisa Kilimo Wilaya ya Misungwi Chirspine Shami ili mmea uweze kustawi vema unatakiwa kupandwa kwa upana wa mita 60 na urefu mita 30.
Aidha, Shami amewataka wakulima kujitokeza kujiandikisha kupata ruzuku ya mbegu na mbolea inayotolewa na Serikali ili kuongeza uzalishaji wa mazao.
Soma zaidi : Nini hatma ya wakazi wa mikoa 10 maskini zaidi Tanzania?
Katika hotuba aliyoiwasilisha bungeni mwezi Mei mwaka huu, Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe, alibainisha kuwa katika kipindi cha mwaka 2022/23, Wizara ya Kilimo ilipanga kuzalisha tani 350,000 za pamba ambapo hadi kufikia AprilI 2023 tani 173, 677 zilikuwa zimezalishwa.
Kwa mujibu wa TCB takriban ekari 1,500,000 hupandwa pamba kila msimu huku zao hilo ambalo huitwa dhahabu ya kijani ikishiriki kuchangia upatikanaji wa fedha za kigeni ambapo mwaka 2019/20 ilichangia Dola milioni 243 za Marekani sawa na Sh608.7 bilioni za Tanzania.
Latest