Bei ya mahindi yapanda Dodoma

July 27, 2020 11:47 am · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Imepanda kutoka Sh61,000 hadi Sh70,000 katika kipindi cha wiki moja. 
  • Wafanyabiashara mkoani watapata faida ya Sh9,000 kwa kila gunia moja la kilo 100. 

Dar es Salaam. Wafanyabiashara wa mahindi katika Mkoa wa Dodoma leo watalala na tabasamu baada ya bei ya jumla ya zao hilo kupanda kwa Sh9,000 ndani ya kipindi cha wiki moja. 

Takwimu za mazao makuu ya chakula zilizotolewa leo (Julai 27, 2020) na Wizara ya Viwanda na Biashara zinaonyesha kuwa bei ya juu ya gunia la kilo 100 la zao hilo linauzwa kwa Sh70,000 katika soko la Majengo mkoani humo.

Bei hiyo imepanda kutoka Sh61,000 iliyorekodiwa Jumatatu Julai 20,2020, sawa na kusema wafanyabiashara wataweka kipindoni Sh9,000 kwa kila gunia moja watakalouza leo sokoni. 

Pia takwimu hizo ambazo hutolewa mara tatu kwa wiki, zinaonyesha kuwa bei ya chini ya mahindi mkoani humo imepanda hadi Sh64,000 kutoka Sh53,000 iliyorekodiwa wiki iliyopita katika soko la Kibaigwa. 

Kwa bei hizo zinazotumika leo, itakuwa ni maumivu kwa wanunuzi na kicheko kwa wafanyabiashara ambao kupanda kwa bei za mazao ndiyo faida kwao. 

Licha ya kuwa bei ya juu na chini ya mahindi katika Mkoa wa Dodoma kupanda, bei ya juu kabisa ya zao hilo inayotumika leo kwa upande wa Tanzania Bara imerekodiwa mkoani Katavi ambayo ni Sh100,000 huku bei ya chini ni Sh45,000 katika Mkoa wa Ruvuma.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW