Kina cha maji Ziwa Victoria chazidi kuongezeka, wananchi watahadharishwa
- Mei mwaka 2020 wastani wa kina cha maji ziwani ulikuwa mita 1134.27 lakini kwa mwaka huu wa 2021 kimefikia mita 1134.87.
- kuongezeka kwa kina hicho kumesababisha nyumba, mashamba na miundombinu kuzingirwa na maji.
- Serikali yawataka watu kuondoka maeneo hayo.
Mwanza. Kufuatia kuongezeko kwa kina cha maji cha Zwa Victoria, Serikali imetoa tahadhari kwa watu wanaoishi kando ya ziwa hilo na kuwataka kuchukua hatua ikiwa ni pamoja na kufanya usafi wa mazingira, kupanda miti na kuepuka shughuli za kibinadamu kando ya ziwa.
Kwa mujibu wa Afisa Habari wa Bodi ya Bonde la Ziwa Victoria, Gerald Itembu, mwezi Mei mwaka 2020 wastani wa kina cha maji ziwani ulikuwa mita 1134.27 lakini kwa mwaka huu wa 2021 kiwango kimeongezeka kwa 0.60 na kufikia mita 1134.87 ambazo hazijawahi kufikiwa katika kipindi chote.
“Hiki ni kipimo kikubwa kuwahi kurekodiwa tangu Bodi ya Bonde la Ziwa Victoria kuanza kurekodi taarifa zake miaka 50 iliyopita” amesema Itembu wakati akizungumza na waandishi wa habari jana Juni 4 jijini Mwanza.
Kutokana na kipimo hicho ni dhahiri kuwa maji hayawezi kupungua kirahisi badala yake yanaendelea kuongeza kadiri mvua zinavyozidi kuongezeka.
Itembu amesema watu wasilaumu maji yamewavamia katika maeneo yake isipokuwa yanafuata asili yake.
Amewataka watu waliokuwa au wanaofanya shughuli karibu na ziwa hilo kuchukua hatua ya kuondoka maeneo hayo huku akiwataka kutunza mazingira ili kuhakikisha hawafanyi shughuli ambazo ni hatari kwenye vyanzo vya maji.
Anasema kinachofanyika kwa sasa ni kufanya kipimo pale maji yalipofikia kutoka usawa wa bahari ili kutoa tahadhari kwa wananchi.
“Hii itasaidia kupunguza athari za kimazingira zinazoweza kutokea,” amesema.
Soma zaidi:
- Usafirishaji mazao ya misitu ya kupandwa sasa kuwa usiku na mchana
- Ushuru wa mazao ya misitu wawaweka matatani viongozi Tanga, Njombe
Madhara yaliyotokea baada ya kina cha maji kuongezeka ni pamoja na makazi ya watu na mashamba kuzungukwa na maji hasa katika mikoa ya Kagera, Mwanza na Mara.
leo Juni 5, Umoja wa Mataifa (UN) kupitia shirika lake la mazingira la UNEP unazindua muongo wa Umoja wa Mataifa wa mrejesho wa mfumo wa ikolojia ulioharibika wakati dunia ikiadhimisha Siku ya Mazingira.
Hii ina maana miaka 10 ya kurejesha hali ya mazingira iwe angani, ardhini au majini.
Latest