Katambi aagiza kusitishwa kwa muda, mikutano vyama vya siasa Tanzania
- Lengo la uamuzi huo ni kuimarisha ulinzi na usalama wa nchi
Arusha. Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi amemuagiza Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Camilius Wambura, kusitisha utoaji wa vibali vya mikutano ya hadhara kwa vyama vyote vya siasa, ili kuimarisha ulinzi na usalama wa nchi.
Katambi ametoa agizo hilo leo Juni 26, 2026, bungeni jijini Dodoma alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Dodoma Mjini, Paschal Kinyere aliyetaka kujua mipango ya Serikali kudhibiti mandamano yalipangwa kufanyika nchini.
“Kupitia Bunge lako tukufu ninamwelekeza IGP Wambura kusitisha utoaji wa vibali vya mikutano ya hadhara kwa kipindi hiki kwa vyama vyote vya siasa, iwe Chama Cha Mapinduzi au chama kingine chochote,” amesema Katambi.
Agizo hilo linakuja ikiwa ni siku chache baada ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kutangaza maandamano ya nchi nzima yakilenga kushinikiza kufufuliwa kwa mchakato wa Katiba Mpya pamoja na kuachiliwa kwa Mwenyekiti wa chama hicho, Tundu Lissu, ambaye anakabiliwa na kesi ya uhaini.
Baada ya kusambaa taarifa kuhusu maandamano hayo, Jeshi la Polisi lilitoa tahadhari likisema hayajapata kibali na kwamba hatua za kisheria zitachukuliwa kwa mtu yeyote atakayeshiriki au kuyaratibu kinyume cha sheria.
Akifafanua sababu za agizo hilo, Katambi amesema Serikali imebaini kuwepo kwa viashiria vya matishio ya kiusalama katika maeneo mbalimbali nchini na kwamba baadhi ya watu wamekuwa wakitumia mikutano ya hadhara pamoja na mitandao ya kijamii kuchochea uvunjifu wa amani.
Amesema vyombo vya ulinzi na usalama vinaendelea kukusanya ushahidi dhidi ya watu wanaodaiwa kuhusika na vitendo hivyo, huku akisisitiza kuwa wale watakaobainika kuvunja sheria watahojiwa na kufikishwa mahakamani.
Waziri huyo pia amewataka wananchi kuendelea na shughuli zao za kila siku, akieleza kuwa Serikali imejipanga kuhakikisha amani na usalama vinaendelea kuimarishwa nchini.