Dawa mseto siyo tiba ya Uviko-19

August 3, 2021 12:10 pm · TULINAGWE ALSON
Share
Tweet
Copy Link
  • Hakuna uthibitisho kuwa dawa mseto inatibu Corona.
  • Dalili za muathirika wa kirusi kipya zinafanana na zile za malaria.
  • Watu wanashauriwa kuendelea kufuatilia taarifa zinazotolewa na vyanzo sahihi.

Dar es Salaam. Kama wewe ni miongoni mwa watu wanaoamini kuwa dawa ‘mseto’ inayotumika kutibu ugonjwa wa malaria inaweza pia kukuokoa dhidi ya Corona (Uviko-19) fahamu umedanganywa na unajiletea madhara zaidi.

Katika mitandao ya kijamii ikiwemo Whatsapp, kuna ujumbe umekua ukisambaa kuwa mgonjwa mwenye maambukizi ya virusi vya Corona anaweza kupona kwa kunywa dawa mseto ya malaria. Hiyo siyo sahihi kwa mujibu wa wataalam wa afya.

Sehemu ya ujumbe huo unaosambaa unasomeka; “Suala la mseto nilisikia kwa mdogo wangu Mwanza, kuwa waliugua karibu mtaa mzima hilo eneo lake la biashara, waliotumia mseto walipona in a week(ndani ya wiki moja)”


Ni kweli dawa hiyo ni tiba ya Uviko-19?

Dk Frank Minja kutoka hospitali ya Hindu Mandal anasema hakuna uthibitisho kuwa dawa ‘mseto’ inatibu Corona ingawa mgonjwa mwenye maambukizi ya ugonjwa huo hupata dalili zinazofanana na mgonjwa wa malaria. 

“Haijathibitishwa kuwa hiyo dawa inatibu Corona. Dalili ya hiki kirusi kipya zinafanana na zile za malaria hivyo mtu anaweza kupona malaria na kudhani amepona Corona,” amesema Dk Frank.

Dalili zinazotajwa kumpata mgonjwa mwenye maambukizi ya Corona wimbi la tatu ni kukauka mate mdomoni, kupata vipele mikononi na miguuni na kuharisha.

Pia kuganda kwa damu kwenye mishipa ya moyo kunakosababisha oksijeni kutosambazwa mwilini na mara nyingi kusababisha kifo cha ghafla.

Dk Frank ameshauri endapo mtu anahisi kupata dalili mojawapo kati ya zilizotajwa aende hospitali kupima ili kupata ufumbuzi na siyo kutumia dawa bila maelekezo ya daktari.

Ifahamike kuwa mpaka sasa, Shirika la Afya Duniani (WHO) halijaidhinisha dawa yoyote kwa ajili ya kitibu Corona, licha ya kurusuhu matumizi ya chanjo sita ikiwemo Moderna na Johnson & Johnson kwa ajili kumkinga mtu na ugonjwa huo.

Enable Notifications OK No thanks