Hapana: Kipimo cha Uviko-19 hakipimi magonjwa mengine
- Kipimo hicho kimetengenezwa kupima virusi aina ya SARS-COV-2 vinavyosababisha ugonjwa wa Uviko-19.
- Hakigundui magonjwa mengine ya mfumo wa upumuaji kama mafua.
Dar es Salaam. Kama wewe ni mmoja wa waliosikia taarifa zinazosambaa mtandaoni kuwa kipimo cha Uviko-19 kinapima magonjwa mengine ya mfumo wa upumuaji taarifa hizo sio za kweli.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) kipimo cha Uviko-19 kimetengenezwa kupima uwepo wa virusi aina ya SARS-COV-2 vinavyosababisha ugonjwa wa Uviko-19.
Kipimo hicho ni kile ambacho mtu anaingizwa puani ili kupata sampuli zinazotumika kugundua kama mtu ameambukizwa au la!.
“Vipimo vya Uviko-19 havigundui homa ya mafua au magonjwa mengine ya mfumo wa upumuaji, vinagundua uwepo wa virusi vinavyosababisha ugonjwa wa Uviko-19 tu,” amesema Dk Phionah Atuhebwe,Afisa Chanjo kutoka WHO.
Mpaka sasa virusi vya Uviko-19 vinapimwa kwa kuchukua sampuli kutoka kwenye pua au mdomo wa mgonjwa jambo linaloleta maswali mengi kwa wagonjwa wa mafua kuwa huenda wakakutwa na virusi hivyo.
Soma zaidi:
-
Hapana: Chanjo ya Uviko-19 haisababishi homa ya monkeypox
-
Mwanza kuchanja watu milioni 1.8 ifikapo Desemba?
Tofauti kati ya mafua na Uviko-19
Kwa kipindi cha miaka mitatu tangu kuingia kwa ugonjwa wa Uviko-19, ugonjwa wa mafua umehusishwa na virusi vya Corona kwa namna mbalimbali.
Licha ya magonjwa hayo kufanana, Kituo cha Magonjwa na Kinga cha nchini Marekani(CDC) kimesema magonjwa hayo yana utofauti mkubwa.
Ripoti ya WHO iliyotolewa Septemba 22, 2022 imeonyesha utofauti uliopo kati ya magonjwa hayo ikiwemo aina za virusi vinavyosababisha magonjwa hayo.
“Uviko-19 unasababishwa na virusi vya SARS-COV-2 na mafua yanasababishwa na maambukizi ya virusi vya mafua,” inasema ripoti hiyo.
Licha ya dalili za magonjwa haya kufanana kituo hicho kimeweka wazi kuwa mara nyingi vipimo vyake ni tofauti.
Hata hivyo, kituo hicho kinashauri mgonjwa kuzungumza na watoa huduma ili kupata vipimo vya magonjwa yote mawili kabla ya kuendelea na matibabu.
Latest
