Rais Rais Samia ataka mapitio gharama Sh27,000 kuunganisha umeme
- Gharama ya Sh27,000 kwa kila Mtanzania haina uhalisia.
- Ameagiza gharama zisiwe juu bali ziwe katika kiwango ambacho Mtanzania anaweza kumudu.
Dar es Salaam. Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amemwagiza Waziri wa Nishati, January Makamba kusimamia urejeshwaji wa gharama za umeme katika hali ya kuzingatia uhalisia na siyo Sh27,000 kwa kila Mtanzania kama ilivyokuwa awali.
Rais Samia ameeleza leo Januari 4, 2022 wakati wa hafla ya kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa matumizi ya fedha za maendeleo kwa ustawi wa Taifa na mapambano dhidi ya Uviko-19 Ikulu jijini Dar es salaam kuwa gharama zilizopo hazina uhalisia na kulisababishia mzigo Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).
Mkuu huyo wa nchi amesema gharama za Sh27,000 hazikuwa za uhalisia na zilisababisha ugumu kwa Tanesco kufikisha umeme kwa Watanzania kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo ukosefu wa nguzo na vifaa.
“Kuna maeneo lazima gharama ya umeme ibebe uhalisia. Unapompangia leo Tanesco aende akaunge umeme kwa Sh27,000 kwa kila mtu yeye anatoa wapi hizo fedha? Hana pa kuzitoa. Lazima aunge umeme kwa gharama inayopaswa kwa kila pahali,” amesema Rais Samia.
Soma zaidi:
- Ndugai na deni la Taifa: Nimekosa mimi, nimekosa sana
- Rais Samia ateua Mwenyekiti mpya wa Tume ya Uchaguzi
- Wizi wa mafuta reli ya kisasa wamkera waziri
Licha ya agizo hilo, Rais Samia amesema, kuna maeneo gharama itabaki hiyo iliyowekwa ili kuwabeba Watanzania hasa kwa sehemu za vijijini na maeneo mengine gharama irudi pale pale.
“Ile sera yetu ya kule vijijini kabisa tuendelee nayo,” amesema Rais Samia akieleza kuwa kaamua kumsaidia Makamba kulieleza jambo hilo.
Ameagiza Wizara ya Nishati kuweka gharama zinazoendana na uhalisia ambazo hazitakuwa juu sana bali ambazo mtu anaweza kuzimudu kuunga umeme.
Bei ya kuunganishwa umeme ya Sh27,000 kwa sehemu za mjini na vijijini ilitangazwa na aliyekuwa Waziri wa Nishati, Dk Medard Kalemani ambapo aliagiza bei hizo zitumike tangu Juni 2021.
“Bei ya kuunganisha umeme wa njia moja iwe kijijini au mjini ni Sh27,000 tu toka Sh177,000 ya awali na wenye kuhitaji kuunganishiwa umeme wa njia tatu, gharama yake ni Sh139,000 kutoka shilingi 912,000 ilivyokuwa ikitozwa awali,” alisema Dk Kalemani.
Latest