UNCHR, UNICEF zawalilia watoto wakimbizi kutoka Ukraine
- Maelfu ya watoto kutoka Ukraine walisaka hifadhi katika nchi jirani wiki iliyopita.
- Watoto hao wapo hatarini kukumbwa na ukatili na manyanyaso.
- UNCHR, UNICEF yatoa wito kwa nchi zinazowapokea watoto hao kuwasajili na kuwapatia ulinzi.
Dar es Salaam. Shirika la kuhudumia wakimbizi (UNCHR) pamoja na Shirika la kuhudumia watoto (UNICEF), wametoa wito kwa nchi ambazo watoto kutoka Ukraine wamekimbilia, kuwasajili na kuwapatia ulinzi.
Mashirika hayo yamesema kuwa watoto wanaovuka mipaka bila uangalizi wa wazazi au walezi wako hatarini kukumbwa na ukatili, manyanayaso, kutumikishwa na kusafirishwa kiharamu.
Jambo hilo limeongeza wasiwasi kwa mashirika hayo na wadau mbalimbali wa masuala ya watoto na hivyo kuomba Serikali zihakikishe kuwa zinawapatia watoto na familia zao njia salama za kupita wakati wanakimbia ghasia.
Zaidi ya wakimbizi milioni 1 kutoka Ukraine walisaka hifadhi katika nchi mbalimbali wiki iliyopita, huku maelfu ya wakimbizi hao wakiwa ni watoto.
Hali hiyo imefanya mashirika hayo kutaka watoto hao na familia zao wanapoingia katika nchi nyingine wapatiwe eneo salama na waunganishwe na mifumo salama ya kitaifa.
Soma zaidi:
-
Mjue askari aliyekataa kubeba silaha vitani na kuokoa watu 75 kwenye pambano kali
-
ICC yaelekeza macho yake Ukraine, Urusi ikiendelea na mashambulizi
-
UN yakwaa kisiki kuiwajibisha Urusi uvamizi Ukraine
Aidha, kwa wale ambao wamekimbia na kuvuka mipaka bila wazazi wao, mashirika hayo yamesema kuwa Serikali ziwajumuishe kwenye mifumo ya kijamii ya malezi ya watoto.
“Tumepata taarifa kuwa baadhi ya taasisi zinataka kuhamishia watoto hao nchi jirani kwa ajili ya usalama. Wakati tunatambua hilo kwamba linafanyika kwa misingi ya kibinadamu, maslahi ya watoto ya kuwa na wazazi na walezi wao lazima yazingatiwe,” wamesema Mkurugenzi Mtendaji wa UNICEF Catherine Russell pamoja na Kamishna Mkuu wa UNCHR, Filippo Grandi.
Hadi Machi 6, jumla ya wakimbizi milioni 1.7 kutoka Ukraine walikimbilia nchi mbalimbali duniani, tangu nchi yao kuvamiwa na Urusi Februari 24 mwaka huu.